1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ishara ya ugumu wa kuundwa serikali

Sudi Mnette
5 Machi 2018

Matokeo ya awali ambayo yametolewa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Italia yanaonesha muungano wenye kufuata siasa za wastani za mrengo wa kulia unaongoza kwa asilimia 37 katika matokeo ya uchaguzi Italia

https://p.dw.com/p/2thnJ
Italien Wahl 2018 | Rechtes Parteienbündnis laut Prognosen vorn | Berlusconi
Picha: Getty Images/P. Marco Tacca

Vuguvugu la  Nyota Tano likipata kiasi cha asilimia 31, huku muungano wa siasa za wastani za mrengo wa kushoto ukiachwa mbali kabisa kwa asilimia 23.

Pasipo muonekano wa ushindi wa wazi wa wingi wa kura kwa kundi lolotea katika uchaguzi huo, matokeo ya mapema leo yanathibitisha matarajio ya mazungumzo ya kuunda serikali itakayokuwa na imani ndani ya bunge kuwa ya muda mrefu na magumu. Matokeo hayo yanaonesha wenye kufuata siasa za mrengo wa kati kulia, wanaopinga wahamiaji na chama kinachopinga sera za Umoja wa Ulaya cha Matteo Salvini yamemshangaza kiongozi wa chama cha Forza Italia, waziri mkuu wa zamani wa Italia  Silvio Berlusconi.

Nafasi ya Matteo Salvini

Italien | Rede des Lega Nord-Vorsitzenden Matteo Salvini in Mailand
Mgombea Matteo SalviniPicha: Reuters/T. Gentile

Chama cha Matteo Salvini kimepata asilimia 18, wakati Forza Italia kikiwa na chini ya asilimia 14. Kwa matokeo hayo yanathibitisha kushindwa kwa vyama viwili ambavyo vilikuwa vinatamba katika siasa za Italia-Forza Italia na cha mrengo wa kati kulia. 

Anna Maria Fiorini mwananchi wa kawaida nchini Italia anayazungumzia matokeo ya awali. "Salvini ni wewe ni mkuu! Nimempigia kura tatu. Sijali lolote, Salvini anataka kufanya jambo kwa taifa lakini Berluscon anapaswa kujiweka kando kwa sababu anahitaji serikali lakini hana uwezo kwa hilo. Berluscon, nakupenda lakini toa nafasi kwa Salvini!"

Mkazi mwingine nchini humo Giuseppe Bruni anasema: "Kile tunachtarajia ni mkwamo wa kisiasa. Serikali inahitajika, hatuwezi kuwa na imani na serikali ambayo haina serikali. Tupo katika mikono ya rais na matakwa ya vyama vya siasa ili kuweza kuunda serikali ya pamoja."

Kwa ujumla wananchi wa Italia wamekuwa na hisia mchanganyiko baada ya matokeo ya awali kuonesha kuwa wapiga kura wamesababisha bunge lenye kuyumba, baada ya uchaguzi huo wa jana Jumapili kwa kuvipa kisogo vya kijadi na kuiingiza katika rekodi miungano ya kisasa na makundi yenye misimamo mikali.

Hadi katika hatua inayotajwa kuwa nusu ya kuhesabu kura, inaonekana kuwa hakuna kati ya makundi makubwa matatu ya kisiasa nchini humo yenye uwezo wa kuunda serikali peke yake na huku kukiwa na matarajio finyu ya kurejea kwa serikali kuu. Jambo hilo linatajwa kuwa ni hatua nyingine chungu  kwa Umoja wa Ulaya kwa mwenendo wa msukumo wa mambo katika utekelezaji wa majukumu yake.

Muungano wa wenye kufuata siasa za mrengo wa kulia unajumuisha ule wa waziri mkuu wa zamani wa Italia Silvio Berlusconi Forza Italia, umeibuka na wingi wa kura mbele ya harakati za vuguvugu la Nyota Tano, ambazo ufuasi wake unaonekana kuashiria kuelekea kuwa chama chenye nguvu  zaidi nchini Italia.

Mwandishi: Sudi Mnette APE/RTR
Mhariri: Yusuf Saumu