1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiYemen

Ufaransa yakamata shehena ya silaha zikielekea Yemen

John Juma
2 Februari 2023

Maafisa wa Marekani wamesema jeshi la majini la nchi hiyo limekamata silaha zikiwemo bunduki, risasi na makombora katika Ghuba ya Oman, wanazodai zilikuwa zinatoka Iran kuelekea kwa waasi wa Kihouthi nchini Yemen.

https://p.dw.com/p/4N1Gq
Jemen angebliche Festsetzung iranisches Schiff mit Waffen
Picha: Reuters/Media Office Of Saudi-led Coalition In Yemen

Picha zilizotolewa na kamandi hiyo pia zinaonesha jeshi la majini la Ufaransa limekamata shehena kama hizo kupelekwa Yemen. 

Ukamataji huo ulifanyika Januari 15 katika Ghuba ya Oman, sehemu ya bahari inayounganisha mlango wa bahari wa Hormuz kwenye Ghuba ya Uajemi, Bahari ya Arabuni na Bahari ya Hindi.Muungano wa kijeshi nchini Yemen wafanya mashambulio dhidi ya waasi wa Houthi

Kamandi kuu ya Marekani imesema miongoni mwa silaha zilizokamatwa ni pamoja na bunduki 3,000, na risasi 578,000. Picha za kamandi hiyo zimeonesha makombora 23 pia yaligunduliwa kwenye shehena nyingine iliyohusishwa na Iran.

Kamandi hiyo imeeleza kuwa ukamataji huo ulifanyika katika njia ambazo kihistoria hutumika kusafirisha silaha kimagendo kutoka Iran hadi Yemen.

Jarida la Marekani la Wall Street limeripoti kuhusu ukamataji huo na kusema vikosi maalum vya Ufaransa ndivyo vilivyozikamata silaha hizo.

Jeshi la Ufaransa halikutoa jibu mara moja lilipoulizwa kutoa kauli kuhusu tukio hilo.

Jemen | Schiff von Houthi Rebellen gekapert
Silaha zilizokamatwa na waasi wa Kihuthi mwaka 2022Picha: HOUTHI MEDIA OFFICE/REUTERS

Japo Iran haikukiri mara moja kuhusu ukamatai huo, picha za silaha ambazo zimetolewa na kamandi ya kijeshi ya Marekani zimeonesha zikifanana na zile zilizokamatwa na vikosi vya Marekani kwenye shehena nyingine ambazo pia zilihusishwa na Iran.

Tangazo hilo linajiri wakati Iran inakabiliwa na shinikizo zaidi kuhusu hatua ya kuipa Urusi ndege zake zisizohitaji rubani katika vita vyake nchini Ukraine na dhidi ya ukandamizaji wake wa waandamanaji nchini mwake kwa miezi kadhaa sasa.

Mvutano wa kikanda pia umeongezeka baada ya ndege isiyohitaji rubani inayoshukiwa kuwa ya Israel kushambulia karakana ya kijeshi iliyoko katikati ya mji wa Isfahan nchini Iran.

Mizunguko iliyopita ya machafuko tangu kuvunjika kwa mkataba kati ya Iran na mataifa yenye nguvu zaidi ulimwenguni kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran, yameisababisha jamhuri hiyo ya Kiislamu kufanya mashambulizi baharini ya kulipiza kisasi.Watu milioni 8 huenda wakakosa misaada Yemen mwezi ujao

Kwa muda mrefu Iran imekanusha kuwapa waasi wa Kihouthi nchini Yemen silaha. Hii ni licha ya nchi za magharibi, wataalam wa Umoja wa Mataifa na washirika wengine kufuatilia na kubaini kuwa zana za kivita kama bunduki na makombora zinazotumika na waasi hao zilitoka Iran.

Makubaliano ya Umoja wa Mataifa yanapiga marufuku kuwapa silaha waasi wa Kihouthi wa Yemen wanaoungwa mkono na Iran. Waasi hao waliukamata mji mkuu wa Yemen Sanaa mwishoni mwa mwaka 2014, na hadi leo wamekuwa kwenye vita na serikali inayotambuliwa kimataifa na inayoungwa mkono na muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia tangu Machi 2015.

Zaidi ya watu 150,000 wameuawa Yemen kufuatia mapigano miongoni mwao wakiwa raia 14,500