1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ufaransa, Marekani kwa kushirikiana na Uingereza zinapanga kukomesha Uharamia katika Pwani ya Somalia.

Scholastica Mazula23 Aprili 2008

Serikali za Ufaransa na Marekani kwa msaada wa Uingereza,zinaandaa azimio katika baraza la usalama litakalo ziruhusu nchi kupambana na uharamia nje ya pwani ya Somalia na kwingineko.

https://p.dw.com/p/DnSL
Manuari ya Ujerumani katika ghuba la AdenPicha: picture-alliance/ dpa

Hayo ni kwa mujibu wa mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Ufaransa.

Ongezeko la uharamia wa majini katika pwani ya Somalia kumelifanya eneo hilo kuwa moja ya sehemu hatari zaidi kwa meli duniani.

Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Ufaransa, Jean-Maurice Ripert, ameliambia shirika la habari la Reuters kwamba Ufaransa kwa kushirikiana na Marekani huku wakiungwa mkono na Uingereza na nchi nyingine wanataka kupambana na uharamia huo.

Bwana Maurice Ripert anasema wameanza kukubaliana juu ya muundo na vielelezo vya kisheria vya azimio hilo .

Maharamia wa kisomali wameiteka nyara meli iliyokua njiani kutoka Dubai jumatatu iliyopita.Hispania imesema imetuma manuari ya kivita baada ya meli ya uvuvi ya nchi hiyo iliyokua na watu 26 ndani yake kushikiliwa katika fukwe za Somalia.

Maharamia hao hawaonyeshi kama wametishwa na wanajeshi wa Ufaransa waliowakamata maharamia sita wa kisomali wiki iliyopita,baada ya kuiteka nyara meli ya anasa ya Ufaransa na kuwashikilia mateka watumishi wake kwa karibu wiki nzima.Maharamaia hao wamepelekwa Ufaransa ili kuhojiwa.

Mwanadiplomasia mmoja wa magharibi kutoka baraza la usalama la umoja wa mataifa,amesema waingereza wanaandaa mswaada wa azimio utakaoshauri kuwepo wanajeshi zaidi wa umoja wa mataifa nchini Somalia,ambako nchi nyingi zinasita kutuma wanajeshi wa kulinda amani.

Jean -Maurice Ripert amesema kuna masuala tete ya kisheria yanayohusika na kuratibiwa mswaada huo wa azimio dhidi ya maharamia,lakini anasema wanaweza kuratibu mswada wa azimio hilo hadi wiki hii itakapomalizika.

Fikra ni kutoa ujumbe,kuzitolea mwito nchi wanachama wa Umoja wa mataifa ziwaandame maharamia kwa kuanzishwa doria,kujibu visa vya uharamia na kupitisha hatua kadhaa za kinga.Amesema bwana Ripert anaehofia ikiwa hatua hazitachukuliwa,basi hali itazidi kua mbaya.

Visa vya uharamia na utekaji nyara vimegeuka kua njia nono ya kujitajirisha na wasomali wengi wanawatendea vyema mahabusi wao wakitegemea kulipwa.

Richard Grenell,msemaji wa tume ya Marekani katika umoja wa mataifa amesema hili ni suala muhimu na wanataka kulipatia ufumbuzi haraka iwezekanavyo.