1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UEFA yamteuwa katibu mkuu mpya

4 Machi 2016

Chama kinachosimamia mashirikisho ya kandanda Ulaya – UEFA kimemtangaza Theodore Theodoridis kuwa kaimu katibu mkuu kuchukua mikoba kutoka kwa rais mpya wa FIFA Gianni Infantino

https://p.dw.com/p/1I7YE
Schweiz Nyon neue UEFA-Generalsekretär Theodore Theodoridis
Picha: Getty Images/AFP/F. Coffrini

Lakini kimesisitiza kuwa uamuzi kuhusu atakayemrithi Michel Platini kama rais hautachukuliwa hadi kesi zake za rufaa zitakapokamilika. UEFA itaandaa mkutano wake mkuu mnamo Mei 3 mjini Budapest, lakini imesema huenda mkutano maalum pia ukaandaliwa kabla ya Juni 10.

Wakati huo huo, mfumo wa teknolojia ya kuthibitisha goli utatumiwa katika fainali za msimu huu za Champions League na Europa League. Pedro Pinto, ni afisa wa mawasiliano wa UEFA "Kuhusiana na teknolojia ya kuthibitisha goli, ambayo mnafahamu itaanzishwa katika mashindano ya Champions League na Europa League kuanzia msimu ujao, itatumiwa katika fainali za mwaka huu za UEFA Champions League mjini Milan na UEFA Europa League mjini Basel.

Mfumo huo wa teknolojia unaothibitisha kama mpira umevuka mstari wa langoni au la, uliidhinishwa na Bodi ya Kimataifa ya Shirikisho la Kandanda – IFAB mwaka wa 2012. Unatumiwa na ligi za nchi za Ulaya na pia ulitumika katika Kombe la Dunia 2014.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/reuters
Mhariri: Yusuf Saumu