1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi wa rais waakhirishwa hadi december 7 Libnan

Oummilkheir30 Novemba 2007

Jenerali Michel Sleiman huenda akakubaliwa na pande zote nchini Libnan

https://p.dw.com/p/CV3H
Jenerali Michel SleimanPicha: AP

Uchaguzi wa rais umeakhirishwa kwa mara nyengine tena jana usiku nchini Libnan,lakini ufumbuzi hauko mbali kufikiwa baada ya mmojawapo wa vigogo wa upande wa upinzani,Michel Aoun kuunga mkono shauri la kuchaguliwa kiongozi wa jeshi Michel Sleiman kua rais nchini humo.

Kikao cha bunge kilichokua kiitishwe leo kumchagua rais,kimeakhirishwa kwa mara ya sita,mara hii hadi December sabaa ijayo,”ili kurahisisha mashauriano ya kufikiwa maridhiano ya jina la mtetezi”hayo ni kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na ofisi ya spika wa bunge Nabih Berri.

Libnan haina rais tangu alipong’oka madarakani Emile Lahoud,baada yam hula wake kumalizika usiku wa mamani wa November 23, baada ya wabunge wanaodhibiti wingi wa viti,wakiungwa mkono nna nchi za magharibi na wa upande wa upinzani wanaoungwa mkono na Syria na Iran kushindwa kuwafikiana nani achaguliwe kua rais.

Muda mfupi baada ya kutangazwa kwamba kikao cha leo kinaakhirishwa,kiongozi wa chama cha Mrengo huru wa kizalendo-CPL,Michel Aoun amesema anaunga mkono jenerali Michel Sleiman,mkuu wa vikosi vya wanajeshi wa Libnan-mtu anaetajwa na wengi ndani ya kambi zote mbili kua na nafasi nzuri ya kuchaguliwa,japo kama mwenyewe hajatamka bado kama anataka kutetea wadhifa wa rais au la.

Akiulizwa maonib yake na waandishi habari,Michel Aoun ambnae binafsi aliwahi kutuma maombi ya kua rais alisema:

“Sitopinga kwasababu nnataka kupendekeza rais awe anachaguliwa na wananchi.Na kwa wakati huu tulio nao,nnakiri,sitopinga maridhiano yaliyofikiwa.”

Jenerali huyo wa zamani ,mshirika mkubwa wa Hisbollah anasema hata hivyo kuna vizingiti vya kikatiba ambavyo vinabidi viondolewe,akihoji serikali iliyoko si halali.”

Katiba itabidi ifanyiwe marekebisho ili jenerali Michel Sleiman aweze kuchaguliwa,kwasababu,kifungu nambari 49 cha katiba hakiruhusu afisa wa ngazi ya juu kuteuliwa kua rai,ila kama atajiuzulu miaka miwili kabla.

Kwa hivyo serikali inabidi iwasilishe mswaada wa marekebisho ya katiba bungeni.Lakini serikali ya waziri mkuu Fouad Siniora inatajwa na upande wa upinzani kua si halali tangu mawaziri wa kishiya walipojiuzulu November mwaka jana.

Jumatano iliyopita serikali ya waziri mkuu Fouad Siniora ilipendekeza jina la jenerali Sleiman ili kumaliza mzozo na kusema wako tayari kuridhia katiba ifanyiwe marekebisho.

Hisbollah walisema watakubali jenerali Sleiman atetee wadhifa wa rais kama Michel Aoun pia ataridhia.

Kwa mujibu wa katiba wadhifa wa rais hukabidhiwa mkristo wa madhehebu vya maronite,waziri mkuu hutakiwa awe wa madhehebu ya sunni na spika wa bunge mshiya.

Tangu alipoteuliwa kuongoza jeshi mwaka 1998,jenerali Sleiman amefanikiwa kuleta umoja jeshini na kujiweka kando na mapambano ya kuania madaraka yanayoleta mfarakano miongoni mwa vyama vya kisiasa nchini Libnan.