1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uchaguzi Ethiopia

Halima Nyanza24 Mei 2010

Wakati kura zikihesabiwa, upinzani nchini Ethiopia umeulalamikia muungano ulioko madarakani unaoongozwa na Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Meles Zenawi kufanya udanyanyifu katika uchaguzi wa bunge uliofanyika jana nchini humo.

https://p.dw.com/p/NVe0
Waziri Mkuu wa Ethiopia, Meles Zenawi, ambaye anatarajiwa kubaki tena madarakani, baada ya uchaguzi wa jana wa Bunge.Picha: AP
Kiongozi wa muungano wa upinzani nchini Ethiopia wa Medrek, Merara Gudina, ameyaelezea matukio kadhaa yanayohusishwa na udanganyifu wakati wa zoezi hilo la upigaji kura katika mji wa kusini wa Oromiya ambao ndio ngome kuu za upinzani pamoja na mji wa Ambo. Amesema haukuonesha kama ni uchaguzi, hata kwa viwango vya Afrika na kwamba hakuna sheria yoyote inayowalazimisha wao kukubali matokeo yoyote na kuongeza kwamba anazotaarifa kuwa visanduku vya kupigia kura viliongezwa. Katika uchaguzi uliopita wa mwaka 2005 rekodi iliyowekwa na vyama vya upinzani ilionekana kuwa nzuri zaidi, hali ambayo ilipelekea kutokea ghasia zilizosababisha vifo vya watu 200, huku serikali ikichukua hatua kali zilizosababisha viongozi muhimu wa upinzani kutupwa gerezani, kukimbilia uhamishoni na wengine kumalizwa nguvu zao kisiasa. Naye Mwenyekiti wa sasa wa muungano huo wa upinzani, Beyene Petros, amesema ushindi unaweza kutangazwa tu, kupitia wizi wa kura na si vinginevyo. Kwa upande wake, kiongozi wa waangalizi wa uchaguzi huo kutoka Umoja wa Ulaya,Thijs Bergman, ameupongeza uchaguzi huo kwa kuwa na amani na utulivu, huku tume ya taifa ya uchaguzi nchini humo ikisema kuwa hakuna ushahidi wowote wa udanyanyifu uliofanywa licha ya viongozi wa upinzani katika majimbo kadhaa kulalamikia kufanyiwa mizengwe.
Thijs Bergman
Kiongozi wa waangalizi wa Uchaguzi kuzoka Umoja wa Ulaya, Thijs Bergman,katika uchaguzi uliofanyika jana Ethiopia.Picha: DW
Hata hivyo, mkuu huyo wa waangalizi wa uchaguzi wa Umoja wa Ulaya amesema wamesikia kilio hicho cha upinzani na kwamba wanafanyia uchunguzi madai hayo. Umoja wa Ulaya umetuma waangalizi wake wapatao 160 katika uchaguzi huo wakati Umoja wa Afrika wakipeleka waangalizi 60, ambapo wapiga kura wapatao milioni 32 jana walichagua wabunge 547 na madiwani. Matokeo  ya majimbo yatatangazwa kesho huku matokeo rasmi ya mwisho yakisubiriwa kutangazwa katika mwezi mmoja ujao.
Wahl in Oromia Äthiopien 23.Mai 2010
Wa Ethiopia wakipiga kura.Picha: DW
Katika nchi hiyo ambayo viongozi wengi mashuhuri wa upinzani wako gerezani na mashirika ya haki za binadamu yakikosoa kutokana na kunywea uhuru wa kisiasa wakati wa kampeni, Waziri Mkuu wa Ethiopia, Meles Zenawi, amepuuza malalamiko hayo yaliyotolewa na upinzani na kusema kuwa anategemea kupata ushindi ili kuendelea kuuimarisha uchumi wa wa nchi hiyo. Mwandishi Halima Nyanza(afp) Mhariri: Miraji Othman