1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ubaguzi wachacha mashariki ya Ujerumani kuelekea uchaguzi

13 Agosti 2009

Mwanasiasa mweusi mzaliwa wa Angola apewa vitsho na chama cha siasa za mrengo wa kulia katika jimbo la Thuringia

https://p.dw.com/p/J9Dw
Mwanasiasa wa chama cha CDU mzaliwa wa Angola asifika kwa kuwajumuisha wageni katika jimbo la ThuringiaPicha: picture alliance/dpa

Hivi karibuni chama cha NPD kilitangaza kitisho dhidi ya mwanasiasa mweusi wa chama cha Christian Demokratic CDU katika jimbo hilo la mashariki mwa Ujerumani.

Chama kikubwa cha mrengo wa kulia cha NPD nchini Ujerumani kilitangaza waziwazi kitisho dhidi ya mwanasiasa wa chama cha CDU katika jimbo la Thuringia ambaye ni mzaliwa wa Angola Zeca Schall.Mwanasiasa huyo mweusi amekuwa akiishi nchini tangu mwaka 1988 na katika kipindi cha hivi karibuni amekuwa akionekana katika mabango ya wagombea wa chama cha CDU katika uchaguzi mkuu kwenye jimbo hilo.

Chama cha CDU kinachoongozwa na Kansela Angela Merkel kimechukua hatua ya kutoa mwito wa kuanzishwa kesi ya uhalifu dhidi ya chama cha NPD kikisema kwamba chama hicho kimekiuka haki ya kikatiba kwa muhusika kutokana na kuidhalilisha hadhi yake.

Udo Voigt, Vorsitzender der NPD
Kiongozi wa chama cha NPD, Udo Voigt-Chama hicho kinakosolewa kwa kueneza siasa za chuki dhidi ya wageniPicha: picture alliance/dpa

Chama cha NPD kilichapisha taarifa yake yenye maandishi ya kibaguzi yanayosema na hapa tunanukuu'' Mtu Mweusi,Mfanyikazi wa kigeni nenda nyumbani kwenu'' mwisho wa kunukuu taarifa ya NPD .

Pia chama hicho kimeonekana katika kipindi cha hivi karibuni kujaribu kuongeza hisia za chuki dhidi ya wageni.Na cha kutia wasiwasi zaidi kundi la chama hicho cha mrengo wa kulia kimetoa mwito kwa wanachama wake katika eneo hilo kuufikisha ujumbe huo kwa Schall binafsi.

Schall ni miongoni mwa wagombea katika eneo hilo kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa utakaofanyika mnamo Agosti 30, akitajwa kuwa mtaalamu wa masuala ya kuwajumuisha wageni kutokana na kutambulika kwa kazi yake.

Schall amezungumzia juu ya kadhia hiyo wakati akihojiwa na gazeti moja akisema hatotishwa na wanachama wenye itikadi kali wa chama hicho cha mrengo wa kulia na juu ya hilo akaongeza kusema-

''Kwangu ilikuwa ni kitendo cha kushtuwa.Sijawahi kukumbana na hali kama hiyo maishani.Ni mara moja kiasi miaka minane au tisa nimewahi kushuhudia hali kama hii wakati nikijaribu kumsaidia mwenzangu mmoja kutoka msumbiji ambaye alikuwa akishambuliwa njiani.Na hapo nilingilia kati kutaka kuzuia na mmoja wa washambuliaji akanijia kwa upande wa nyuma na kunigonga na kuangushwa chini na niliumia kidogo.''

Aidha mwanasiasa huyo mwenye asili ya kiafrika ambaye kwa sasa yuko chini ya ulinzi wa polisi amepania kuendelea na kampeini za uchaguzi akiwa pamoja na wanachama wenzake wa CDU ambao pia wamesema wanamuunga mkono hadi mwisho wa safari yao.

Polisi katika eneo la Thuringia wameanzisha utaratibu wa kuchunguza uhalifu katika kesi hiyo kwa kile walichosema ni kukiukwa kwa haki ya mtu binafasi ya kuwa na hadhi ya kibinadamu.Hajo Funke ni mwenyekiti wa masuala ya kisiasa na utamaduni katika chuo kikuu cha Berlin amekisifu chama cha CDU kwa hatua iliyoichukua lakini pia ameonya kwamba chama cha NPD kisipuuzwe-

''Kwavyovyote vile wanawawakilisha wengi walio na msimamo dhahiri wa siasa kali katika mrengo wa kulia na makundi ya mrengo wa kulia na kwa mantiki hiyo hilo halijakwisha.Halijakwisha kabisa ukitazama masuala mengine.Kwamfano juu yakuongezeka kwa matumizi ya nguvu kwa walio na itikadi kali na ghasia ni mambo yaliyoshamiri mwaka jana.Kwa hivyo kuna dalili ya wazi kabisa kwamba kuna jambo linaloendelea chini kwa chini katika jamii ambayo inahusika na suala la ubaguzi na inahusiana na kutuhumiwa kwa wenye siasa kali za mrengo wa kulia.Kwahivyo tusipuuze hatari iliyopo katika suala zima la utamaduni wetu wa kisiasa.Sio hatari kwa bunge la taifa,lakini ni hatari katika uchaguzi wa baadhi ya majimbo na hasa katika eneo la mashariki ya Ujerumani''

Ripoti ya mwaka 2008 iliyotolewa na shirika la ndani la ujasusi inasema kwamba chama hicho cha NPD katika jimbo la Thuringia kiko katika hali ya kusambaratika kikitilia maanani kupunguwa kwa idadi ya wanachama wake.

Mwandishi:Wood Tanya/Saumu Mwasimba

Mhariri Abdul-Rahman.