1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tshisekedi akataa mageuzi ndani ya mhimili wa mahakama

Sylvia Mwehozi
30 Juni 2020

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi amekataa mageuzi yoyote yatakayodhoofisha uhuru wa mahakama.

https://p.dw.com/p/3eYSm
Kongo | Präsident Felix Tshisekedi
Picha: Presidence RDC/G. Kusema

Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi, amekataa mageuzi yoyote ndani ya mhimili wa mahakama, akisema yatadhoofisha uhuru wake na kuathiri msingi wa kanuni zinazosimamia haki.

Kumekuwepo na hali ya kutoelewana katika muungano tawala juu ya mapendekezo yaliyotolewa ya kufanya mabadiliko, hususan kuipatia nguvu zaidi wizara ya sheria katika kushughulikia mashitaka ya uhalifu. Tofauti hizo zilisababisha wiki iliyopita kukamatwa kwa muda mfupi, waziri wa sheria na kusababisha waziri mkuu kutishia kujiuzulu kwa serikali.

Katika hotuba yake kwa taifa ya kuadhimisha miaka 60 ya uhuru wa taifa hilo kutoka mikononi mwa Ubelgiji, Tshisekedi amegusia mgogoro huo, akisema hakubaliani na mageuzi yoyote. Rais huyo aliingia madarakani Januari 2019, na kuunda ushirika na Kabila ambaye bado ana nguvu kupitia wingi wa viti bungeni, baraza la mawaziri na ofisi ya waziri mkuu.

Chanzo: rtre