1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Trump amteua Bolton kuwa mshauri wake mpya wa usalama

Sylvia Mwehozi
23 Machi 2018

Rais wa Marekani Donald Trump amemuondoa mshauri wake wa usalama wa taifa H.R McMaster na kumteua katika nafasi hiyo John Bolton, mtu mwenye msimamo mkali na aliyewahi kuwa balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa.

https://p.dw.com/p/2updt
USA neuer Sicherheitsberater John Bolton
Picha: picture-alliance/Zumapress/M. Brochstein

Trump kama kawaida alitumia ukurasa wake wa Twitter kutoa tangazo hilo la karibuni la mabadiliko ya watumishi, hatua ya mbayo inauweka katika mashaka makubwa mustakabali wa makubaliano ya kihistoria kuhusu mpango wa nyukilia wa Iran.Hii ni mara ya tatu kwa Trump kubadilisha mshauri wake wa usalama wa taifa. 

"Ninafuraha kutangaza kwamba kuanzia tarehe 9 mwezi wa 4 balozi John Bolton atakuwa mshauri wangu mpya wa usalama wa taifa" aliandika Trump. Tangazo hilo linakuja siku chache baada ya kumuondoa aliyekuwa waziri wa mambo ya nje Rex Tillerson, na kumuweka mkurugenzi wa shirika la ujasusi la CIA Mike Pompeo ambaye pia ana msimamo mkali kuelekea Iran.

H.R. McMaster
H.R McMaster mshauri wa sasa wa usalama wa taifaPicha: picture-alliance/Newscom

Trump amemsifu McMaster kwa utumishi wake na kusema kwamba ataendelea kuwa rafiki yake. McMaster alitarajiwa kuondoka baadae mwaka huu, kwahiyo kuondoka kwake hakukuwa na mshangao. Lakini uteuzi wa Bolton umeishtusha Washington.

Ni mtu aliyepigia chapuo vita vya Iraq, pia aliunga mkono mashambulizi ya awali ya silaha za nyukilia dhidi ya Korea Kaskazini na mabadiliko ya utawala nchini Iran, na kumfanya atofautine na Warepublican. Zaidi amezungumzia uteuzi wake akisema, "nafikiri kwamba mshauri wa usalama wa taifa na muundo mzima wa maamuzi ya usalama wa taifa nchini Marekani unalenga kuwa rahisi, unalenga kutekelezeka kwa namna ambavyo rais aliyeko madarakani anapendelea. Kwahiyo marais tofauti wamekuwa na mifumo tofauti".

Uteuzi wake ulikuwa unapingwa vikali na wengi wanaomzunguka Trump, hususan maafisa wa kijeshi walioshuhudia ukatili wa vita kwa macho yao.

Bolton, veterani wa utawala wa George W. Bush, atakuwa na jukumu kubwa katika kuunda sera ya nje ya Marekani, akiwa muamuzi wa mijadala baina ya majasusi wa Marekani, wanajeshi na wanadiplomasia.

USA CIA Director Mike Pompeo wird als Außenministernachfolge gehandelt
Mike Pompeo aliyeteuliwa karibuni kuwa waziri wa mambo ya nje Picha: Reuters/Y. Gripas

Lakini jukumu lake kubwa zaidi litakuwa ni kutengeneza maamuzi ya usalama ambayo yanafika katika dawati la Trump. Mtizamo wake wa kiitikadi juu ya nguvu ya Marekani unaendana na ule wa Trump, ingawa wawili hao hawajawahi kukubaliana kuhusu vita ya nje.

Mjumbe mmoja wa Republican, akizungumza kwa sharti la kutotajwa jina alikiri kuwepo wasiwasi juu ya uteuzi wake. Hapa Bolton amegusia masuala muhimu atakayoyapa kipaumbele akisema, "nadhani masuala yanayotukabili ni kuenea kwa silaha na ugaidi, haya ni masuala niliyo shughulika nayo kabla. Rais bila shaka anayo kwenye orodha ya vipaumbele vyake. Kwa hiyo ndio tutafanyia kazi, miongoni mwa mengine mengi".

Tofauti na mawaziri wa mamabo ya nje au ulinzi, mshauri wa usalama wa taifa anawajibika moja kwa moja kwa rais na haihitaji kuthibitishwa na Seneti ili kuchukua wadhifa wake.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AFP

Mhariri: Iddi Ssessanga