1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania yaadhimisha siku ya wanawake duniani

8 Machi 2022

Tanzania ni kama sehemu nyengine duniani leo imeadhimisha siku ya wanawake huku ikijivunia mafanikio kadhaa yaliopatikana kwa wanawake tokea nchi hizi mbili Tanzania na Zanzibar kupata uhuru wake.

https://p.dw.com/p/48B9L
Tansania l Neue Präsidentin Samia Suluhu Hassan
Picha: AP/picture alliance

Rais wa Jamhuri wa muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alikuwa mgeni katika kilele cha sherehe hizo.

Mambo ambayo yanaonekana kutajwa kuwa ni miongoni mwa mafanikio ni kupanda kwa nafasi ya mwanamke katika uongozi, kujikomboa wanawake kiuchumi na kupatikana nafasi za wanawake kwenye harakati za maendeleo pamoja na kuimarisha mifumo ya sekta za elimu ya afya.

Changamoto kubwa iliyopo ni kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ambayo kwa kiasi kikubwa inaonekana kuwaathiri wanawake zaidi hasa katika kilimo na uzalishaji wa mwani baharini.

Athari za janga la corona 

Tansania Präsidentin  Samia Suluhu Hassan
Picha: Eric Boniphase/DW

Akihutubia taifa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametaja janga la ugonjwa wa Covid 19 kuwa limeirejesha nyuma dunia kiuchumi hasa katika bara la Afrika huku akisifu uamuzi wa kutofunga milango wakati wa wimbi hilo.

soma Janga la Covid-19 limepora haki za wanawake na wasichana

Maadhimisho hayo ambayo yamewashirikisha viongozi wa serikali zote mbili Tanzania na Zanzibar, viongozi wa dini, wanasiasa, mashirika ya kimataifa na mabalozi mbali mbali pamoja na wanaharakati na taasisi zilizo mstari wa mbele kupigania haki za wanawake.

Awali akisoma risala ya wanawake katika maadhimisho hayo yaliyofanyika katika uwanja wa Mautsetung,  Afisa Muandamizi wa Serikali ya Zanzibar, Bi Sharifa Abeid  amesema hali ya Tanzania na Zanzibar ni ya kujivunia kutokana kutolewa nafasi kubwa kwa wanawake akianzia Rais mwenyewe kuwa ni mwanamke, mawaziri, makatibu wakuu wakurugenzi na maafisa mbali mbali ambao wanaopewa nafasi za uongozi na kuzitumia kwa ufanisi mkubwa.

Aidha alitaja harakati za wanawake kuwa zinazidi kuimarika kwa kuungwa mkono na serikali na hakuacha kutaja vikwazo vya mabadiliko ya hali ya hewa ni moja ya changamoto kubwa kwa wanawake katika kutofikia malengo waliojiwekea.

soma Rais Samia akutana na wanawake kuadhimisha siku ya Demokrasia

Mashirika ya kimataifa, wanadiplomasia na mabalozi wanaofanya kazi zao hapa nchini wametoa salamu zao katika maadhimisho hayo na kuonesha namna ambavyo wanaridhishwa na uamuzi wa Tanzania kumpa nafasi mwanamke pamoja na maendeleo ya kiuchumi. miongoni mwao ni balozi wa Finland

Burudani za ngoma za asili, ziliwainua wanawake na viongozi kitini na kuwasogeza uwanjani kucheza akiwemo mwenyewe Mama Samia.

Maadhimisho hayo yaliohudhuriwa na viongozi mbali mbali wa serikali zote mbili mawaziri na viongozi wengine na kilichowavutia watu zaidi ni kuonekana kwa Mama Salma Salim mke wa aliyekuwa Rais wa Zanzibar Dk Salmin Amour Juma.

 

 

Salma Said DW; Zanzibar