1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania: Maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru wa Tanganyika

George Njogopa9 Desemba 2019

Maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru wa Tanganyika yamefanyika leo mjini Mwanza na kuhudhuriwa na rais John Pombe Magufuli. Kwa mara ya kwanza chama cha upinzani Chadema pia kimeshiriki kwenye maadhimisho hayo.

https://p.dw.com/p/3US1U
Tansania Feier 58 Jahre Unabhängigkeit
Picha: DW/D. Bulendu

Chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, Chadema kwa mara ya kwanza leo kinashiriki sherehe za maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanganyika ikiwa ni hatua ya aina yake. Chama hicho kimekuwa kikisusia sherehe hizo tangu mwaka 2015 ulipofanyika uchaguzi mkuu kama ishara ya kupinga matokeo ya urais wa wakati huo. 

Kushiriki kwa Chadema kwenye sherehe hizi kunatuma ujumbe mpya kuhusu siasa za Tanzania hasa wakati ambapo hamasa ya kuelekea kwenye uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2020 ikiwa ni mada inayojadiliwa na kila chama.

Chadema ambayo imekuwa ikisizusia sherehe hizi inajumuika na viongozi wa serikali na wale wa chama tawala cha CCM katika wakati ambapo vigogo wakuu waliojiunga na chama hicho wakati wa vuguvugu la uchaguzi uliopita wakiwa wamejiondoa ndani ya chama hicho wengine wakirejea kwenye chama chao kilichowakuza CCM.

Ingawa hatua hii ya Chadema kushiriki kwa mara ya kwanza tangu ulipomalizika uchaguzi uliopita, imewavutia wengi wakidadisi sababu zilizopo nyuma ya pazia, hata hivyo baadhi ya wachambuzi wa mambo wanasema kuwa huenda chama hiki kinaanza kuweka mguu sawa kuelekea uchaguzi ujao.

Baadhi ya watumbuizaji wakati wa maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru wa Tanganyika
Baadhi ya watumbuizaji wakati wa maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru wa TanganyikaPicha: DW/D. Bulendu

Hoja hiyo inapata mashiko na kauli ya chama hicho kinachosema kwamba hakioni sababu ya kuendelea kujiweka kando na sherehe hizo kwa vile kinajiandaa kushika dola katika uchaguzi ujao. Mkurugenzi wa itifaki na mambo ya nje ya chama hicho, John Mrema, amesema suala la chama hicho kuamua kushiriki sherehe za mwaka huu ni tafsiri inayoakisi mwelekeo mpya wa chama hicho kuelekea siasa za usoni.

Wakati Chadema kikijumuika na viongozi wengine wa chama na chama tawala, CCM kwenye maadhimisho hayo, chama kingine cha upinzani ACT-Walendo kimesusia sherehe hizo kwa madai kuwa hakioni sababu ya kushiriki wakati hakuna uhuru wa maoni, demokrasia kuzidi kubanwa na vyama vya upinzani kuendelea kuandamwa na dola.

Afisa habari wa chama hicho, Suphiani Juma amesema hizo ni baadhi ya sababu za msingi zinazokifanya chana hicho kususia sherehe hizo.

Katika sherehe hizi, Chadema imeongozwa na mwenyekiti wake, Freeman Mbowe aliyeambatana na wabunge kadhaa.