1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Stuttgart yaweka hai matumaini ya kubaki katika Bundesliga

Bruce Amani
4 Machi 2019

Timu mbili za Bundesliga zimetoa mifano miwili inayotofautiana kuhusu thamani ya kuwabadilisha, au kuendelea kuwapa muda makocha katika mapambano ya katikati ya msimu ya kuepuka kushuka daraja.

https://p.dw.com/p/3EPnG
Fußball Bundesliga VfB Stuttgart - Hannover 96
Picha: Imago/J. Huebner

Timu mbili za Bundesliga zimetoa mifano miwili inayotofautiana kuhusu thamani ya kuwabadilisha, au kuendelea kuwapa muda makocha katika mapambano ya katikati ya msimu ya kuepuka kushuka daraja. Stuttgart, ambayo iliamua kubaki na Markus Weinzierl licha ya kupata pointi mbili tu katika mechi nane, waliwabamiza Hannover 5 – 1 Jumapili.

Hannover walitumai kuwa na mabadiliko chini ya kocha mpya Thomas Doll, lakini sasa wamepata vipigo vinne katika mechi tano tangu aliporejea katika Bundesliga baada ya kufunza kandanda la nje ya Ujerumani.

Hannover waliamua kufanya mabadiliko ya kocha, kwa kumtimua mtangulizi wa Doll Andre Breitenreiter mnamo Januari 27 baada ya mechi nane bila ya ushindi.

Katika mechi nyingine, Werder Bremen ilipata pointi moja muhimu dhidi ya nambari saba kwenye ligi Wolfsburg, kwa kutoka sare ya 1 – 1.

Bundesliga - Borussia Moenchengladbach gegen Bayern München
Bayern sasa wana pointi sawa na DortmundPicha: Reuters/T. Schmuelgen

Lakini kilichozungumzwa sana mwishoni mwa wiki ni ushindi mnono wa Bayern Munich wa 5 – 1 dhidi ya Borussia Moenchengladbach ambao ni ujumbe mkali katika kinyanganyiro cha ubingwa wa ligi msimu huu. Mabingwa hao walitumia fursa ya kichapo cha Borussia Dortmund cha 2 – 1 dhidi ya Augsburg. 

Katika mechi ya Bayern, mshambuliaji wa Poland Robert Lewandowski alikuwa na sababu nyingine ya kusherehekea. Mabao yake mawili dhidi ya Gladbach, yalifikisha mabao yake ya Bundesliga kuwa 195, sawa na mkongwe wa Werder Bremen Claudio Pizarro na kuwafanya kuwa wafungaji bora zaidi wa kigeni katika historia ya Bundesliga.

Na wakati Bayern wakiwa na matumaini kuwa sasa wanaweza kubeba ubingwa wa saba mfulilizo, mambo yalikuwa mabaya kabisa kwa Schalke 04. Schalke ambao ni makamu bingwa wa msimu uliopita, sasa wako katika nafasi ya tano kutoka mkiani. Walibamizwa 4 – 0 na Fortuna Düsseldorf.

Kwingineko, RB Leipzig iliimarisha matumaini yake ya kucheza kandanda la Champions League msimu ujao, baada ya kuwafunga Nuremberg 1 – 0. Leipzig sasa wako nafasi ya tatu, pointi mbili mbele ya Gladbach. Eintracht Ushindi wa Frankfurt wa 3 – 2 dhidi ya Hoffenheim na wa Bayer Leverkusem wa 2 – 0 dhidi ya Freiburg unahakikisha kuwa timu hizo zinawania nafasi za kandanda la Ulaya.