1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Stuttgart mabingwa wapya wa Bundesliga

21 Mei 2007

Stuttgart imeiambia Schalke kutangulia si kufika na vishindo vyenu vya darini vya muda mrefu kileleni mwa Bundesliga,vimesishia sakafuni jumamosi.

https://p.dw.com/p/CHcB
VFB Stuttgart na taji laubingwa 2007
VFB Stuttgart na taji laubingwa 2007Picha: AP

Naam, kutangulia kweli si kufika,kwani firimbi ya mwisho ilipolia juzi jumamosi,si Schalke iliongoza Bundesliga muda mrefu wala Werder Bremen ilikua nyuma yake kipindi kipindi kirefu iliotoroka na ubingwa,bali VFB Stuttgart,timu ya kusini ya Ujerumani ambayo mpambano 1 kabla ya mwisho ikiongoza kwa pointi 2.

Stuttgart iliilaza jumamosi Cottbus mabao 2:1,lakini ilikua Cottbus iliotangulia kutia bao na kuwafanya mashabiki wa Stuttgart kupigwa na homa ya wasi wasi.Mkwaju mkali lakini aliouchapa Thomas Hitzlsperger na bao la ushindi la Sami Khedira yalitosha kuitawaza Stuttgart tena mabingwa wa Ujerumani.

“Kishindo tulichotiwa kilikua kikubwa mno hii leo.Ilikua kazi ngumu na timu yetu ilipatwa na matatizo.Cottbus ilitupa changamoto kubwa kabisa.”-Alisema Horst held, meneja wa Stuttgart.

Schalke kwa mara nyengine tena imeibuka makamo-bingwa baada ya kuilaza Bielefeld mabao 2:1.Hii ni mara ya 3 Schalke 04 inamaliza makamo-bingwa.

Na huko Uingereza mambo yalikuwa vipi ?

Didier Drogba wa Chelsea,aliufumania mlango wa Manchester united hapo jumamosi kwa bao lake katika finali ya kwanza ya kombe la FA kuchezwa katika uwanja mpya wa Wembley.Drogba kwa kweli aliwanyima Manchester nafasi ya kutoroka na mataji yote 2-ubingwa na kombe la FA.Hii ni mara ya kwanza kwa Chelsea kutwaa Kombe la FA.

Changamoto hii ya kukata na shoka haikuangaliwa kwa shauku kubwa huko Uingereza tu bali hata Afrika mashariki.Nchini Kenya ilikua asie na mwana aeleke jiwe na yule asiekua na mguu ,alitia gongo mkutano mikahawani na mitaani mbele ya rundinga:

Eric Ponda anaripoti kutoka Mombasa:

Wakati Mamelodi Sundawons ya Afrika Kusini imekata tiketi yake ya duru ijayo ya Kombe la shirikisho la dimba la afrika kwa kumudu suluhu bao 1:1 na Gafsa ya Tunisia , mabingwa wa Tanzania, Young Africans wameshindwa tena kufua dafu mbele ya Al-Merreikh ya Sudan baada ya kukomewa mabao 2:0.

Katika medani ya riadha-msichana wa Ethiopia, Meseret Defar jana aliweka rekodi mpya yxa dunia ya masafa ya maili 2 wakati wa mashindano ya Adidas Track Classic huko California.Defar, bingwa wa Olimpik wa mita 5000, aliivunja rekodi ya zamani ya dakika 9:11.97 iliowekwa na Regina Jacobs wa Marekani 1999.Muda wake ni dakika 9.10.47.