1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Somalia kuisaidia Somaliland baada ya soko kuteketea moto

Grace Kabogo
4 Aprili 2022

Waziri Mkuu wa Somalia, Mohamed Hussein Roble ameamuru dola milioni 11.7 zitolewe kwa ajili ya kuisaidia Somaliland kutokana na moto mkubwa ambao umeliteketeza soko la Wahen lililoko mjini Hargeisa.

https://p.dw.com/p/49QDx
Somaliland I Großbrand auf dem zentralen Markt in Hargeisa
Picha: Mataan Yuusuf/AFP/Getty Images

Roble amesema fedha hizo ni msaada wa kimataifa uliotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya jimbo la Somaliland ambalo lilijitangazia uhuru wake kutoka kwa Somalia.

Viongozi wa wafabiashara wa Somaliland pia wameahidi kuchangia ili kusaidia kulijenga upya soko hilo.

Rais wa Somaliland, Muse Bihi Abdi amesema amezungumza kwa njia ya simu na Rais wa Somalia, Mohamed Abdullahi Farmajo na Waziri Mkuu Roble kuelezea masikitiko yao kutokana na moto huo.

Kundi la al-Shabaab lenye mafungamano na mtandao wa kigaidi wa al-Qaeda, pia yameelezea kusikitishwa na moto huo. Meya wa Hargeisa, Abdikarim Ahmed Mooge amesema wafanyabiashara katika soko hilo wamepoteza mali yenye thamani ya dola bilioni mbili.