1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Msumbiji yabanwa kutekwa mwandishi wa Rwanda

Yusra Buwayhid
2 Juni 2021

Chama cha Wakimbizi wa Rwanda nchini Msumbiji kimelaani kutoweka kwa mwandishi wa habari raia wa Rwanda, Ntamuhanga Cassien, ambaye alikuwa uhamishoni katika kisiwa cha Inhaca, katika mkuu wa Msumbiji, Maputo.

https://p.dw.com/p/3uMIm
Mosambik ehemalige RENAMO-Guerillas
Picha: DW/D. Anacleto

Cassien alichukuliwa na watu wanane wasiojulikana ambao walijitambulisha kama maafisa wa Polisi ya Jamhuri ya Msumbiji (PRM). Pamoja nao alikuwa ni raia mmoja wa Rwanda aliyezungumza lugha moja na Cassien.

Lakini msemaji wa Idara ya Kitaifa ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai, Hilário Lole, amedai kwamba hakuna rekodi yoyote ya malalamiko ya kutoweka au kutekwa nyara kwa raia wa Rwanda.

Cleophas Habiyareme msemaji wa chama hicho cha wakimbizi wa Rwanda nchini Msumbuji, alifafanua kwamba malalamiko yalifikishwa kwa Kamishna Mkuu wa Wakimbizi wa Umoja wa Mataifa (UNHCR) huko mjini Maputo.

Soma pia: Viongozi wa SADC wakutana katika mkutano wa dharura

Ntamuhanga Cassien, mwenye umri wa miaka 37, alikuwa mwandishi wa habari na mkurugenzi wa kituo cha redio cha Kikristo "Amazing Grace" mjini Kigali, Rwanda, na ambaye kabla ya kukamatwa kwake alikuwa akifanya kazi kama mfanyabiashara nchini Msumbiji.

Demonstration gegen Entführungen und Krieg in Maputo
Waandamanaji mjini Maputo wakiandamana kupinga matukio ya utekaji nyara, wakiituhumu serikali kwa kutojali, na polisi kwa rushwa.Picha: picture-alliance/dpa

DW imezungumza na mkurugenzi wa Kituo cha Demokrasia na Mendeleo Msumbiji (CDD), Adriano Nuvunga, na kutaka kujua kama kisehria Msumbiji ina haki ya kumkamata mwandishi habari huyo?

"Serikali ya Msumbiji lazima iseme kwa nini imemshikilia. Haiwezi kumzuia kiholela na haiwezi kumhamisha  huru kiholela. Serikali ya Msumbiji lazima iwaambie raia wa Msumbiji na jumuiya ya kimataifa kwanini ilimzuia katika mazingira hayo. Lazima waonyeshe hati ya korti inayoidhinisha polisi kumkamata."

Muhanga wa unyanyasaji wa utawala

Cassien alidai kuwa ni mwathirika wa mateso ya kisiasa kama wakosoaji wengine wa utawala wa Rais wa Rwanda Paul Kagame.

Alitoroka gerezani nchini Rwanda mnamo 2017, baada ya kuhukumiwa kifungo cha hadi miaka 25 gerezani mnamo mwaka 2015, kwa kula njama dhidi ya serikali, kuhusika na makosa ya kigaidi pamoja na mauaji, madai ambyo yalipingwa wakati huo na mashirika ya kutetea haki za binadamu.

Soma pia: Miezi miwili ya shambulio la Palma, manusura bado wanakimbia

Kuna uvumi wa uingiliaji kati wa Rwanda katika mzozo wa jimbo la Cabo Delgado, huko Msumbiji, na kwamba kupotea kwa mwandishi wa habari huyo kulikuwa ni njia ya kuishukuru Rwanda kwa msaada wake.

Ruanda Opposition Musiker  Kizito Mihigo
Mwanamuziki wa upinzani nchini Rwanda, Kizito Mihigo alikamatwa na kukutwa akiwa amekufa gerezani mjini Kigali, katika kile kilichoelezwa na mamlaka kuwa ni kujiua.Picha: STEPHANIE AGLIETTI/AFP/Getty Images

"Inaonekana wazi kukamatwa huku kwa mwandishi habari wa Rwanda kunaweza kuwa sehemu ya ya haya mambo yanayoendelea Msumbiji. Kwa mtazamo huo, Msumbiji inaonekana kuwa mshirika wa Rwanda," alisema Nuvunga.

Chama cha wakimbizi wa Rwanda chatoa wito

Katika taarifa, Chama cha Wakimbizi wa Rwanda nchini Msumbiji kilielezea wasiwasi wake juu ya madai ya visa vya kushikiliwa kiholela kwa raia wa Rwanda nchini Msumbiji.

Soma pia: Wazungu waliokolea kwanza katika shambulizi la Msumbiji

Chama hicho kimesema kwamba kinahitaji kuona uingiliaji kati wa haraka wa Serikali ya Msumbiji, kwani kulingana na sheria mkimbizi ana haki ya kulindwa.

Rais wa Rwanda Kagame aliyeingia madarakani mwaka 1994, anasifiwa kwa kuendeleza nchi hiyo baada ya ghasia za mauaji ya kimbari, lakini pia anashutumiwa kwa kukandamiza uhuru wa kujieleza pamoja na upinzani wa kisiasa nchini mwake.

Chanzo: DW