1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Serikali ya Afghanistan na Taliban wazungumza Doha

12 Septemba 2020

Pande mbili zinazozozana Afghanistan zimeanza mazungumzo ya kihistoria kwa mara ya kwanza Jumamosi kwa kuwaleta pamoja wanamgambo wa Taliban na wawakilishi walioteuliwa na serikali.

https://p.dw.com/p/3iNRU
Katar Doha | Afghanistan Friedensverhandlungen
Picha: Getty Images/AFP/K. Jaafar

Mazungumzo hayo yanalenga kumaliza vita vilivyodumu kwa miongo kadhaa nchini humo.

Mkuu wa ujumbe wa Afghanistan Abdullah Abdullah katika ufunguzi wa mazungumzo hayo amesema lengo lao ni kumaliza miaka 40 ya umwagikaji wa damu, "tumekuja hapa kwa nia njema na lengo zuri la kusitisha umwagikaji wa damu na kupata amani ya kudumu nchi nzima," alisema Abdullah.

Kiongozi wa ujumbe wa ujumbe wa Taliban naye Mullah Abdul Ghani Baradar ameahidi kwamba nchi yake itashiriki mchakato huo wa kutafuta amani kwa uaminifu kamili na kwamba kuwe na subra katika mazungumzo hayo. Baradar amesema kundi lake linalenga kuwepo kwa Afghanistan ya Kiislamu ambayo itakuwa na uhusiano mzuri na nchi zengine katika kanda hiyo na nchi jirani.

"Mchakato wa mazungumzo bila shaka utakuwa na matatizo, tunauhakikishia ulimwengu kwamba tutjaribu kupata matokeo mazuri," alisema Baradar.

Mazungumzo hayo ni muhimu kwa ajili ya amani ya kudumu Afghanistan

Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Mike Pompeo alihudhuria hafla ya ufunguzi iliyofanywa nchini Qatar. Hili ni tukio la hivi karibuni katika msururu wa mambo yanayofanywa na utawala wa Trump kuelekea uchaguzi mkuu wa Marekani mwezi Novemba.

Katar Doha | Afghanistan Friedensverhandlungen | Abdullah Abdullah
Mkuu wa ujumbe wa Afghanistan Abdullah Abdullah(katikati) akiwasili kwa mazungumzoPicha: Getty Images/AFP/K. Jaafar

Mazungumzo hayo ni muhimu kwa ajili ya amani ya kudumu itakayotoa nafasi pia kwa vikosi vya Marekani na Muungano wa kujihami wa NATO kuondoka nchini humo baada ya karibu miaka 19.

Pompeo amedokeza kwamba mazungumzo hayo yanatarajiwa kuwa yenye utata na kwamba matokeo ni ya Waafghanistan na wala si Marekani, "kila mmoja anabeba jukumu kubwa na muna fursa ya kuiacha mivutano yenu."

Pande hizo zilizo kwenye mzozo nchini Afghanistan pia zinatarajiwa kujadili mabadiliko ya katiba na kugawana mamlaka katika mazungumzo hayo ya Doha.

Muungano wa kujihami wa NATO umeisifu hatua ya kuanza kwa mazungumzo hayo ikisema ni "fursa ya kihistoria" huku ukionya kwamba machafuko nchini Afghanistan bado yanasalia kuwa katika kiwango cha juu mno.

"Hii ni fursa ya kihistoria, NATO inasimama na Afghanistan ili hatua zilizopigwa na kuhakikisha nchi hiyo si makao ya magaidi tena," amesema Katibu Mkuu wa NATO Jens Stoltenberg katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter.

Serikali ya Afghanistan imewateua wanawake wanne kuwa miongoni mwa ujumbe wake unaoshiriki mazungumzo

Miongoni mwa wawakilishi walioteuliwa na serikali katika mazungumzo hayo ni wanawakewanne ambao wameapa kuhakikisha haki za wanawake zinaheshimiwa katika mpango wowote wa kugawana madaraka na wanamgambo wa Taliban. Miongoni mwa haki hizo ni kufanya kazi, elimu na kushiriki siasa. Wanawake hawakuruhusisiwa ´kufanya yote hayo katika miaka mitano ya utawala wa Taliban.

Katar Doha | Afghanistan Friedensverhandlungen
Ujumbe wa Taliban ukifuatilia mazungumzo hayo ya amaniPicha: Getty Images/AFP/K. Jaafar

Wanamgambo wa Taliban waliondolewa madarakani na muungano wa majeshi unaoongozwa na Marekani mwaka 2001 kwa kumficha Osama bin Laden.

Mazungumzo haya ya amani yalikuwa yalikuwa yamepangiwa kufanyika Machi 10 ila yalicheleweshwa hadi kumalizika kwa ubadilishanaji wa wafungwa kulikochukua muda mrefu kati ya serikali ya Afghanistan na Taliban.