1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sebastian Vettel awanyamazisha wahakiki

14 Oktoba 2013

Sebastian Vettel amezoea kutawala mashindano wakati anapoanza wa kwanza, lakini ushindi wake ambao alitoka nyuma na kumaliza wa kwanza katika mkondo wa Suzuka nchini Japan, umewanyamaisha wakosoaji wake

https://p.dw.com/p/19zKg
Picha: picture-alliance/dpa

Ushindi wake wa mkondo wa Suzuka nchini Japan, mwishoni mwa wiki umedhihirisha kuwa ushindi wa kila mara wake Vettel hautokani na ubora wa gari lake la timu ya Red Bull.

Mjerumani huyo amekabiliwa na ubezi, na hata kuzomewa na mashabiki mwaka huu lakini kile ambacho hakiwezi kufutwa ni kuwa yeye ni mmoja wa madereva mahiri wa mbio za Formula One.

Vettel amekosolewa kwa kuwafanya mashabiki kutotazama mbio za Formula One, kwa ajili tayari huwa wanajua mshindi atakuwa ni nani, wakati aliposhinda mfululizo mikondo ya Ubelgiji, Italia, Singapore na Korea Kusini, lakini alilazimika kung'ang'ania ushindi wa Japan.

Kama kila kitu kitakwenda sawa, basi Vettel atavikwa taji la bingwa wa dunia katika Formula One kwa mwaka wa nne mfululizo mnamo Oktoba 27 kwenye mkondo wa Indian Grand Prix. Mjerumani huyo anaongoza msururu wa madereva bora akiwa na pengo la pointi 90 mbele ya Fernando Alonso wa timu ya Ferrari, huku ikisalia mikondo minne msimu huu ukikamilika. Alonso tayari amekiri kuwa taji litamwendea Vettel.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/reuters

Mhariri: Yusuf Saumu