1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Saudi Arabia yaipinga ripoti ya Umoja wa Mataifa

Zainab Aziz
30 Agosti 2018

Wataalamu wa masuala ya haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa wametaja mateso na maafa makubwa kwa raia wa Yemen yanayosababishwa na mashambulizi ya anga ya vikosi vya mfungamano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia.

https://p.dw.com/p/3424e
Yemen - al-Hudaida. Soldat
Picha: picture-alliance/dpa/T. Almamari

Kundi la wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanaoshughulikia mgogoro wa Yemen wamesema maelezo yaliyothibitishwa yanaonesha kwamba makundi yayohusika kwenye mgogoro huo na ambayo yanatumia silaha yanaendelea kukiuka haki za binadamu na pia yanatenda uhalifu chini ya sheria ya kimataifa. Wataalamu hao wa Umoja wa Mataifa wamesema baadhi ya mashambulizi hayo yanaweza kuwa ni uhalifu wa vita.

Lakini taarifa iliyochapishwa leo na shirika la habari la Saudi Arabia, SPA, imesema kwamba muungano wa kijeshi unaoongozwa na nchi hiyo unaipinga ripoti hiyo ambayo haikutaja jukumu la Iran katika kuendelea kwa vita nchini Yemen pamoja na msaada wake kwa waasi wa Houthi, licha ya ushahidi wa wazi uliotolewa na muungano huo wa kijeshi kwa vyombo husika vya kimataifa.

Taarifa hiyo imeongeza kusema kwamba ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa si sahihi na pia inapendelea upande mmoja, hivyo basi muungano huo wa kijeshi  unapanga kujibu tuhuma dhidi yake kisheria, ukipinga pia hatua ya kutajwa kwa maafisa wa ngazi za juu kutoka kwenye nchi washirika katika ripoti hiyo.

Raia mmoja wa Yemen aliyejeruhiwa kwenye shambulizi la anga akimbizwa hospitalini
Raia mmoja wa Yemen aliyejeruhiwa kwenye shambulizi la anga akimbizwa hospitaliniPicha: Reuters/A. Zeyad

Kwa upande wake, Marekani imeelezea wasiwasi wake kutokana na ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa inayogusia juu ya uwezekano wa kutendekea uhalifu wa kivita nchini Yemen na imezitaka pande zote zinazohusika zijiepushe na ukiukaji wa haki za binadamu. Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Jim Mattis, amesema nchi yake inazingatia upya misaada inayotoa kwa mfungamano huo wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia:

Hata hivyo,waziri huyo wa ulinzi wa Marekani ameutetea kikamilifu muungano huo kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia na kuungwa mkono na Marekani katika mapambano dhidi ya waasi wa Houthi wanaoungwa mkono na Iran. Mattis ameongeza kusema kuwa msaada wa Marekani una masharti, ya kwamba lifanywe kila linalowezekana kuepuka mgogoro wa kibinadamu na kuunga mkono mchakato wa amani wa Umoja wa Mataifa.

Mwandishi: Zainab Aziz/AFP/DPA

Mhariri: Mohammed Khelef