1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Safari ya tija

17 Januari 2013

Safari hii ya kweli, matunda yake yamea Haioneshi kufeli, wapinzani watopea Haina yake mithili, habari yalingania Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

https://p.dw.com/p/17Lsx
DW Journalist Othman Miraji, mit Kindern in Dar Es Salaam.
50 Jahre Kisuaheli RedaktionPicha: DW

Alinisihi babangu, habari za uhakika
Niwambie na wenzangu, Ujerumani zatoka
Tena ni kwa lugha yangu, Kiswahili zasikika
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Hadi leo sijajuta, ukweli nihadithie
Miaka shirini sita, dunia niitambue
Na bado sijaichoka, niko nayo ina miye
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Kwa makala moto moto, vijana tunajifunza
Kwa magoma na mikito, hakika nyinyi wa kwanza
Mafanikio si ndoto, ni nyendo tumejifunza
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Haki mnosimamia, ukweli mtuambie
Hata iwe ni Korea, tawala zao tujue
Njia gani wapitia, jibu watutangazie
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Kongo mpaka Kenya, kwa Kiswahili mwatamba
 Hamida bila mumunya, Burundi anawapamba
 Uganda sijawaminya, Leila anawabamba
 Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Shangwe mshangilieni, Othmani wa Miraji
Kipindiche cha maoni, nakiona kama taji
Mola mjaze imani, kwetu huyu ndiye gwiji
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Kalamu i mkononi, Mnete u salamuni,
Ssesanga u mdomoni, Umilkheri moyoni
Situmai yu makini, Idi msalimieni
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Hadhi ya wenye imani, iko kwa Mola Azizi
Sitasita kumhini, abisha si wabobezi
Kwingineko sitamani, redio yenu makazi
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Chanda changu ki shidani, kuendelea siwezi
Nawaaga kwaherini, Amina we mtetezi
Radhi ninawaombeni, iwapo nimewaudhi
Nusu karne ya kheri, Mungu awape uhai

Tanbihi: Shairi hili limeandikwa na Mwalimu Shaaban S. J. Lissu wa Dar es Salaam - Tanzania kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 50 ya DW.

Mhariri: Mohammed Khelef