1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Guinea achaguliwa tena kwa muhula wa tatu

Iddi Ssessanga
24 Oktoba 2020

Rais wa Guinea Alpha Conde amechaguliwa tena kuongoza kwa awamu ya tatu baada ya kushinda asilimia 59.49 ya kura kulingana na tume ya uchaguzi nchini humo. Mpinzani wake mkuu Cellou Dalein Diallo amepata asilimia 33.5.

https://p.dw.com/p/3kOGQ
Guinea Präsidentschaftswahlen | Alpha Conde
Picha: John Wessels/AFP

Akitilia mashaka uhuru wa tume ya uchaguzi, Diallo mwenye umri wa miaka 68 alijitangaza mshindi siku ya Jumatatu kabla ya kutolewa kwa matokeo - jambo lililosababisha makabiliano kati ya wauasi wake na vikosi vya usalama.

Waandamanaji waliingia tena mitaani katik mji mkuu Conakry siku ya Jumamosi, na wakaazi wa baadhi ya vitongoji walisema polisi walikuwa wanafyatua mabomu ya machozi kuwatawanya.

Soma pia: Uchaguzi wa Guinea: Rais Alpha Conde awania muhula wa tatu

"Tutakuwa mitaani hadi Cellou Dalein atuombe kurudi nyumbani," alisema moja, aliekataa kutaj jina lke, akimaanisha kiongozi wa upinzani. Diallo aliliambia shirika la habari la AFP kwamba atafungua shauri mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi.

Guinea Präsidentschaftswahlen | Cellou Dalein Diallo
Kiongozi wa upinzani Guinea, Cellou Dalein Diallo ambaye amesema atapinga matokeo ya urais mahakamani na mitaani.Picha: John Wessels/AFP

"Tutapinga udanganyifu huu wa uchaguzi mitaani," alisema. "Lakini bado tutapeleka suala hili katika mahakama ya katiba, bila kuwa na matrajio makubwa."

Wakati tume huru ya uchaguzi nchini Guinea (CENI), ilitangaza matokeo ya awali, mahakama ya katiba inapaswa kuyaidhinisha matokeo hayo. Inatarajiwa kufanya hivyo katika muda wa wiki moja.

Kwa ushindi wake huo, Conde anatazamiwa kuongoza kwa miaka mingine sita, na anaweza kuwania muhula mwingine wa nne baada ya hapo.

Soma pia: Alpha Conde wa Guinea kuwania muhula mwingine madarakani

Upinzani mkubwa dhidi ya muhula wa tatu ulizusha maandamanio kuanzia Oktoba 2019, ambamo vikosi vya usalama viliuwa dazeni kadhaa za watu.

Mnamo mwezi Machi, rais huyo alishinikiza kuandikwa katiba mpya ambayo alihoji kwamba ingeifanya nchi hiyo kuwa ya kisasa zaidi. Hatua hiyo ilimruhusu kuepuka ukomo wa mihula miwili ya marais.

Guinea ni taifa maskini, licha ya kuwa na hifadhi kubwa ya madini ya bauxite, dhahabu na almasi, ambayo ina utulivu mdogo wa kisiasa tangu ilipopata uhuru mwaka 1958.

Conde, mhamasishaji wa zamani wa  upinzani aliekaa miongo kadhaa uhamishoni, alikuwa rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia nchini humo mwaka 2010, na alichaguliwa tena mwaka 2015.

Lakini rais huyo mwenye umri wa miaka 82, anashutumiwa kwa ukiukaji wa haki za binadamu katika muongo mzima wa utawala wake. Na ushindi huo wa muhula wa tatu unaongeza hofu kwamba huenda akawa hana nia ya kuachia madaraka.

Chanzo: Mashirika