1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Rais wa China Xi Jin Ping ataka muungano na Taiwan

Angela Mdungu
9 Oktoba 2021

Rais wa China Xi Jinping leo Jumamosi amesema, muungano wa China na Taiwan ni lazima ufanyike na hilo litatokea kwa njia ya amani. Xi ametoa wito huo licha ya kitisho cha China kukivamia kisiwa hicho

https://p.dw.com/p/41TSb
China - Xi Jinping in Beijing
Picha: Carlos Garcia Rawlins/REUTERS

 Ameyasema hayo wakati wa sherehe rasmi za mdhimisho ya  miaka 110 ya mapinduzi ya mwaka 1911 ambayo yalianzisha Jamhuri ya China. Akizunguza mbele ya wanasiasa, na maafisa wa jeshi, kiongozi huyo wa China ameeleza kuwa kuungana tena kwa njia ya amani kutakuwa kwa maslahi ya taifa zima la China

Rais Xi ametoa wito huo ikiwa ni siku kadhaa baada ya jeshi la China kutuma idadi kubwa ya ndege za kijeshi zilizokuwa zikiruka kuelekea Taiwan katika mazoezi ya kijeshi kitendo ambacho kisiwa hicho kimekiita kuwa ni tishio.  China na Taiwan zilitengana mwaka 1949 wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe, na chama tawala cha kizalendo cha wakati huo kilikimbilia katika visiwa hivyo na kumpa nafasi mkomunisti Mao Zedong kunyakua madaraka upande wa bara.

Bila ya kuitaja Marekani, ambayo imejitolea kusimama kama mlinzi wa Taiwan, Rais wa China Xi Jin Ping alionya mataifa ya kigeni kutokuingilia suala hilo, akisema, "Suala la Taiwan ni suala la ndani ya China. "

Taiwan kufanya maonesho ya kijeshi

Mwaka huu Taiwana itafanya maonesho ya vifaa vya kijeshi ambayo ni nadra kufanyika na miongoni mwa vifaa hivyo ni makombora ya kivita. Jeshi la anga linatarajiwa pia kuonesha ndege za kivita. Maonesho hayo ya kijeshi yatafanyika katika madhimisho ya kitaifa Jumapili mbele ya jengo la ofisi ya Rais katikati mwa mji mkuu, Taipei.  

Hii itakuwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi kuhusisha vifaa vya kijeshi katika maadhimisho hayo na ni mara ya kwanza pia tangu alipoingia madarakani RaisTsai Ing wen mwaka 2016 wakati mvutano kati ya China na Taiwan ulipopamba moto. Vyombo vya habari vya ndani wakati vikiripoti kuhusu ma mazoezi ya maandalizi vilionesha magari makubwa ya kurusha makombora yakiendeshwa katika mitaa ya Taipei, ingawa makombora yenyewe hayakuonekana moja kwa moja.

Taiwan Taipei | Präsidentin | Tsai Ing-wen
Rais wa Taiwan Tsai Ing-wenPicha: Annabelle Chih/Imago Images

Mtaalamu wa masuala ya ulinzi katika taasisi ya utafiti wa sera za taifa wa Taiwan Kuo Yu-jen anasema miaka ya nyuma, serikali ya Taiwan ilifanya siri uwezo wake wa kivita ili kuepuka uchokozi. Lakini tabia iliyooneshwa na China kwa Taiwan hivi karibuni ya uthubutu kupita kiasi imeifanya Taiwan ioneshe kuwa inao uwezo wa kuikabili China

Taiwan ambayo inajiita rasmi Jamhuri ya Uchina (ROC), imekuwa na serikali huru tangu Wazalendo wa China walipokimbilia huko kutoka Bara mnamo 1949 baada ya kushindwa katika za vita vya wenyewe kwa wenyewe vya China walivyokuwa wakipigana na Mkomunisti Mao Zedong.

Tangu kutengana, Taiwan imekuwa ikijitawala lakini China hailitambui hilo na imekataa kuweka pembeni uwezekano wa kutumia nguvu kukiweka kisiwa hicho kwenye himaya yake. Imejaribu pia kuitenga Taiwan kimataifa kwa kuizuia kutambuliwa na Umoja wa Mataifa na mashirika ya kimataifa. Marekani na Japan zimeionya China juu ya ongezeko la vitisho kwa kisiwa hicho na ukanda wote.