1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Tanzania apokea ripoti ya mkaguzi wa hesabu za serikali

Admin.WagnerD30 Machi 2022

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema kumekuwepo na mifumo mingi serikalini bila isiyo na uwiano, iliyotengenezwa kwa madhumuni ya kuchota fedha.

https://p.dw.com/p/49Ejx
Samia Hassan | Präsidentin von Tansania
Picha: Hannah Mckay/AFP/Getty Images

Aidha, kiongozi huyo ameamuru kurejeshwa kwa tozo ya shilingi 100 kwenye nishati ya mafuta, kutokana na matatizo ya kiuchumi ambayo amesema yanatokana na mzozo wa Ukraine. Kauli hiyo imetolewa na Rais Samia wakati akipokea ripoti ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 30,2021.

Rais Samia amesema kuwa kumekuwepo na mifumo mingi serikalini bila mifumo hiyo kusomana huku kila mmoja akitengeneza mfumo utaoruhusu uchotaji wa fedha huku akitangaza  kubaini kutokuwepo na usimamizi wenye weledi serikalini.

Soma zaidi:Rais Samia awakosoa wanaombeza kuhusu miradi ya Magufuli

Akizungumza wakati akipokea ripoti hiyo, kiongozi huyo amegusia mzozo wa kivita kati ya Urusi na Ukraine namna ambavyo umeathiri Nyanja ya uchumi ikiwa ni pamoja na kupanda kwa bei za bidhaa na kuamuru kurejeshwa kwa tozo ya shilingi 100 katika nishati ya mafuta iliyoondolewa katika siku za hivi karibuni.

Awali akiwasilisha ripoti yake mkaguzi mkuu wa serikali Charles Kichere alisema kuwa Deni la Serikali Tanzania limeongezeka kutoka Sh56.76 trilioni mwaka uliopita hadi kufikia Sh64.52 trilioni kufikia Juni 30, 2021. Vile vile mkaguzi huyo amezungumizia kuhusu kutofautiana kwa ankara za mifumo za taasisi za umma namna zilivyosababisha upotevu wa pesa nyingi.

Taarifa hiyo ya mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu ya serikali  ya Tanzania imebeba mambo mengi ikiwa ni pamoja na ushauri kwa serikali.

DW:Dodoma