1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Obama ziarani Canada

Jane Nyingi/ AFPE..Picha AFP19 Februari 2009

Rais Barack Obama kukutana na waziri mkuu wa Canada Stephen Harper

https://p.dw.com/p/GxJz
Rais Barack Obama wa Marekani.Picha: AP

Rais wa Marekani Barack Obama leo anafanya ziara yake ya kwanza ya kigeni tangu alipoingia madarakani kwa kuitembelea Canada.Canada ni mshirika mkubwa wa Marekani kibiashara. kwa siku biashara kati ya mataifa hayo mawili inafikia thamani ya dolla billioni 1.5.


Katika ziara hiyo itakayochukua muda wa saa saba, rais Barack Obama anataraji kukutana na waziri mkuu wa Canada Stephen Harper mjini Ottawa. Maswala yanayotarajiwa kutawala mazungumzo yao ni biashara, mgogoro wa kiuchumi duniani na na jukumu la kikosi cha jumuiya ya kujihami ya nchi za magharibi NATO nchini Afghanistan.


Canada ina wanajeshi elfu 2,700 katika mkoa wa Kandahar, unaotajwa kuwa hatari nchini Afghanistan kutokana na mashambulio ya mara kwa mara ya wanagambo wa Taliban. Huku wanajeshi 108 wa NATO wanaoshika doria nchini humo wakiwa wameauwa na 300 kujeruhiwa, Canada ndio iliyoathirika zaidi na nchi hiyo imetangaza kuwa itawaondoa wanajeshi wake nchini Afghanistan kufikia mwaka 2011. Tayari marekani imetangaza kuwa itapeleka wanajeshi elfu 17 wa ziada nchini Afghnistan kukabiliana na uasi wa Taliban.


Katika ziara hii rais Obama pia anatarajiwa kuwahakikishia Wacanada kuwa hana nia ya kuvunja uhusiano wa kichumi kati ya Marekani na Canada kufuatia hatua ya Marekani ya kuzidi kutaka kujipendelea katika masuala ya kiuchumi.

Huku rais Obama akisisitiza kuwa marekani itazingatia sheria za kimataifa juu ya suala la biashara huru, waziri mkuu wa Canada Stephen Harper,wiki iliyopita alielezea wasiwasi wake kuhusu kipegee cha Marekani kinachotilia mkazo kununuliwa kwa bidhaa za Marekani. Biashara kati ya Marekani na Canada ni ya thamani ya billioni 1.5 kwa siku.


Ziara hii ya rais Barack Obama nchini Canada inatarajiwa kumpa nafasi ya kuimarisha uhusiano wake na waziri huyo mkuu wa Canada ambaye ni rafiki mkubwa wa George Bush aliyeondoka madarakani.


Viongozi hao wawili wanatarajiwa kufanya mkutano na waandishi wa habari baada ya chakula cha mchana ambapo pia swala la ongezeko la joto duniani linatarajiwa kuzunguziwa.Rais Obama anaitaka Marekani kuongoza katika kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa


Rais Obama pia atakutana kwa muda mfupi na kiongozi wa upinzani katika uwanja wa ndege wa Ottawa kabla ya kurejea Marekani.