1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Raia wa Malawi wanamchagua kiongozi wao katika Uchaguzi Mkuu

Mjahida20 Mei 2014

Raia wa Malawi wanapiga kura katika uchaguzi ulio na ushindani mkali, huku rais Joyce Banda,rais wa kwanza wa kike kusini mwa Afrika, akikabiliana na wagombea takriban 12, wanaowania kiti hicho cha urais.

https://p.dw.com/p/1C2zK
Laini ndefu ya wapiga kura nchini Malawi
Laini ndefu ya wapiga kura nchini MalawiPicha: AFP/Getty Images

Takriban watu milioni 7.5 zaidi ya asilimia 90 ya wananchi wamejiandikisha kupiga kura katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika ilio na idadi ya watu milioni 16.7.

Banda anakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa wagombea wengine ikiwa ni pamoja na Peter Mutharika anayetokea chama cha DPP na ambaye ni nduguye rais wa zamani Bingu wa Mutharika pamoja na kasisi Lazarus Chakwera, kutoka chama cha Malawi Congress Party (MCP).

Mgombea watatu kati ya 12 walio katika kinyanganyiro hicho cha kuwania urais ni Atupele Muluzi, mtoto wa rais wa zamani Bakili Muluzi, anayetokea chama cha UDP.

Wagombea wengine1,300 wanashindania nafasi 194 za ubunge ambapo takriban asilimia 70 ya viti hivyo vinatarajiwa kwenda kwa wabunge wapya.

Rais Joyce Banda wa Malawi
Rais Joyce Banda wa MalawiPicha: AFP/Getty Images

Vituo vya kupigia kura vilifunguliwa mapema alfajiri, lakini matatizo ya kiufundi katika eneo la Blantye yakachelewesha zoezi la kupiga kura, hali ilioanza kuzua wasiwasi.

Hata hivyo wapinzani wengi wa Rais Joyce Banda tayari wameanza kulalamika wakidai kuna mpango wa kuiba kura. Ucheleweshwaji wa aina yoyote ule huenda ukasababisha hali ya kutoaminiana katika mchakato mzima wa uchaguzi huu ulio na ushindani mkali tangu kumalizika utawala wa chama kimoja miongo miwili iliopita.

Kumekuwa na matukio ya vurugu katika kituo cha kupigia kura katika shule moja mjini Blantyre, huku mamia ya wapiga kura wakibakia katika kituo hicho kwa saa kadhaa wakati maafisa wa uchaguzi wakisubiri vifaa vya kupigia kura kuwasili katika kituo hicho.

Hata hivyo kwa kukosekana utafiti wa kura ya maoni unaoaminika, wachambuzi wengi nchini humo wanasema chama cha rais Banda cha People kinaonekana kuwa chama kinachopendwa zaidi kutokana na umaarufu wake katika maeneo ya vijijini ambapo rais huyo amekuwa akiendeleza miradi ya maendeleo na ruzuku kwa wakulima.

Mmoja wa wagombea wa kiti cha urais Peter Mutharika
Mmoja wa wagombea wa kiti cha urais Peter MutharikaPicha: Gianluigi Guercia/AFP/Getty Images

Rais Joyce Banda aliingia madarakani miaka miwili iliopita baada ya Bingu wa Mutharika kufariki akiwa bado yupo uongozini.

Aidha waangalizi kutoka Umoja wa Ulaya, Umoja wa Afrika, Jumuiya ya ushirikiano wa maendeleo baina ya serikali za nchi za kusini mwa Afrika SADC pamoja na Jumuiya ya soko la pamoja kwaajili ya Mataifa ya Mashariki na Kusini mwa Afrika COMESA wanuangalia kwa karibu uchaguzi wa Malawi, nchi iliyo na sifa nzuri linapokuja suala la uwazi katika uchaguzi.

Mwandishi: Amina Abubakar/AFPE/DPAE

Mhariri: Yusuf Saumu