1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

OLIMPIA:Mioto ya porini inazidi kuleta mashaka Ugiriki

28 Agosti 2007
https://p.dw.com/p/CBVJ

Watalii pamoja na wakaazi wa maeneo yaliyokumbwa na mioto wanaendelea kukimbia maeneo hayo huku serikali ikiendelea kuongeza juhudi za kupamabana na mioto hiyo pamoja na kutafuta chanzo cha mioto hiyo iliyosababisha kuuwawa kwa watu 63 hadi sasa.

Kundi la kupambana na magaidi nchini Ugiriki limewahoji baadhi ya watu 32 waliokamatwa wanaoshukiwa kuanzisha moto huo kimakusudi.

Ugiriki imekumbwa na mioto tangu ijumaa iliyopita kuanzia eneo la kisiwa cha Evia kaskazini mwa mji wa Athens hadi Peloponnese kusini mwa nchi.

Zima moto wa Ugiriki wakiungwa mkono na kundi kutoka nchi za Umoja wa Ulaya wanaendelea kupambana na moto huo lakini vyama vya upinzani nchini Ugiriki vimeishutumu serikali kwa kushindwa kuikabili hali hiyo.Chama cha upinzani cha PASOK kimeshutumu juhudi za serikali za kukabiliana na hali ya mambo na kusema suala la kuwa mioto hiyo imeanzishwa kwa makusudi na watu fulani ni sababu inayotumiwa na serikali kuficha udhaifu wake.Kiasi cha wafuasi 2000 wa mrengo wa kushoto waliandamana kutoka mjini Athens hadi maeneo ya bunge kuilaumu serikali.

Hali hii inatokea huku kukisalia wiki tatu tu kabla nchi hiyo kufanya uchaguzi wa bunge.