1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Obama atembelea maonyesho ya biashara Hannover

Admin.WagnerD25 Aprili 2016

Rais Barack Obama ametembelea maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover pamoja na Kansela Angela Merkel kabla ya kuwa na mazungumzo na viongozi wa Ulaya juu ya masuala ya dunia na usalama.

https://p.dw.com/p/1Ic7Y
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani wakitembelea maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover. (25.04.2016)
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani wakitembelea maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover. (25.04.2016)Picha: Reuters/W. Rattay

Akizungumza akiwa katika banda la Marekani Rais Obama amesema "kiasi kikubwa sana cha uchumi wetu wa dunia na ukuaji unaozalisha nafasi za ajira unachochewa na mwamko wa ubinifu, ugunduzi, kutunga na baadae kuzigeuza fikra hizo kuwa bidhaa mpya,kuwa kampuni kuw viwanda vipya na huduma mpya mambo ambayo huzalisha ajira nzuri."

Amesema hiyo hii ni fursa nyengine kwake kumwambia kila mtu aje hapo na kununuwa bidhaa zilizotengenezwa Marekani.

Rais Barack Obama wa Marekani akizungumza akiwa katika banda la Marekani leo hii wakati alipotembelea maonyesho hayo ya biashara na viwanda ya Hannover akiandaman na mwenyeji wake Kansela Angela Merkel wa Ujerumani ambapo amesema yuko Hannover kwa sababu ana fahari kuonyesha mwamko wa ubunifu wa Marekani.

Kufunguliwa rasmi kwa maonyesho

Merkel na Obama walifunguwa rasmi maonyesho hayo ya makubwa kabisa ya biashara na viwanda duniani ya Hannover Messe hapo jana.Marekani kwa mara ya kwanza imekuwa nchi mshirika katika maonyesho hayo

Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani wakati wa kufunguwa maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover. (24.04.2016)
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani wakati wa kufunguwa maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover. (24.04.2016)Picha: Getty Images/A. Körner

Wakati wakianza kukaguwa mabanda ya Marekani na Ujerumani katika maonyesho hayo Kansela Angela Merkel wa Ujerumani alitamka kwa Kingereza kwa kuwa utamu wa puding ni kuila basi na waanze.

Obama na Merkel walitembelea vibanda vya Marekani vya kutengeneza mashine za kuchapisha za 3D ,vifaa vya kompyuta na teknolojia ya anga za juu wakiandamana na mkururo wa wapiga picha, waandishi wa habari, maafisa usalama na mawaziri.

Merkel ni mwanasayansi

Obama aliwaambia watu walioko kwenye maonyesho hayo kwamba Kansela Merkel ni mwanasayansi kwa hiyo anaweza kuelewa mambo hayo.Merkel ni mtaalamu wa fizikia.

Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani wakitembelea maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover. (25.04.2016)
Rais Barack Obama wa Marekani na Kansela Angela Merkel wa Ujerumani wakitembelea maonyesho ya biashara na viwanda ya Hannover. (25.04.2016)Picha: Reuters/K. Pfaffenbach

Wakati alipokuwa katika banda moja rais huyo alifanya mzaha kwamba mara atakapokuwa hayuko tena madarakani atatafuta wakati wa kuanza kubuni vitu.

Ziara ya siku mbili ya Obama nchini Ujerumani ni kituo cha mwisho cha ziara yake ya mataifa matatu ambayo ilimfikisha Uingereza na Saudi Arabia.Ziara hii pia inakuja kabla ya kufanyika kwa mkutano wa kilele wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO katika mji mkuu wa Poland Warsaw.

Mkutano mdogo wa kilele

Baada ya hotuba yake kwa viongozi wa biashara Obama ataungana na Merkel kwa mazungumzo juu ya masuala yanayoikabili dunia hivi sasa ambayo pia yatahudhuriwa na Rais Francois Hollande wa Ufaransa, Waziri Mkuu wa Italia Matteo Renzi na Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron.

Mazungumzo hayo ambayo yanatajwa kwa mkutano mdogo wa kilele pia yatagusia mapambano dhidi ya wapiganaji wa Dola la Kiislam nchini Syria na Iraq,mzozo wa wakimbizi barani Ulaya ,mzozo wa Libya, kura ya maoni ya Uingereza juu ya uwanachama wake wa Umoja wa Ulaya na makubaliano ya biashara kati ya Marekani na Ulaya yanayopendekezwa pamoja na hatua za kudhibiti mabavu ya Urusi.

Mwandishi : Mohamed Dahman /dpa

Mhariri : Mohammed Abdul-Rahman