1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

New York. Mazungumzo kuhusu Somalia yakwama.

28 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCfY

Baraza la usalama la umoja wa mataifa kwa mara nyingine tena limeshindwa kukubaliana juu ya taarifa inayotaka kumalizika mara moja kwa mapigano nchini Somalia.

Duru ya pili ya majadiliano ilivunjika kutokana na Qatar kusisitiza kuwa taarifa hiyo iyatolee mwito majeshi ya Ethiopia na majeshi ya mataifa mengine ya kigeni kuondoka majeshi yao kutoka Somalia.

Hilo ni suala ambalo wajumbe wengine 14 wa baraza hilo hawakulikubali.

Hakuna majadiliano mengine yaliyopangwa hivi karibuni. Mjumbe maalum wa katibu mkuu wa umoja wa mataifa katika eneo hilo Francois Lonseny Fall amesema hata hivyo kuwa mzozo huo unapaswa kutatuliwa kwa njia ya mazungumzo.

Hii inakuja wakati majeshi ya Ethiopia pamoja na yale ya serikali yanakaribia katika mji mkuu wa Somalia , Mogadishu, mji ambao ni ngome kuu ya majeshi yanayounga mkono umoja wa mahakama za Kiislamu.

Kituo cha televisheni cha Al –Jazeera kimemnukuu kiongozi wa umoja huo wa mahakama za Kiislamu akisema kuwa majeshi yao yamejiondoa kutoka Mogadishu. Wakati huo huo wanamgambo wa wababe wa vita wameingia mitaani mjini Mogadishu kuchukua udhibiti wa mji huo. Msemaji wa serikali Abdirahman Dinari amesema kuwa majeshi ya serikali yatauchukua mji huo muda wowote katika saa chache zijazo.