1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Nchi za siasa za kizalendo zapoteza mshirika wao Trump?

Bruce Amani
11 Novemba 2020

Serikali za siasa kali za kizalendo Hungary, Poland na nchi nyingine za Umoja wa Ulaya zimepoteza mtu wao kufuatia kushindwa kwa Trump. Zitalazimika kutafakari upya mkakati wao? Itarahisisha siasa katika Umoja wa Ulaya? 

https://p.dw.com/p/3l7a8
USA President Donald Trump trifft ungarischen Premierminister Viktor Orban in Washington
Picha: Imago Images/UPI Photo/K. Dietsch

Makamu wa rais wa zamani Joe Biden alitoa msimamo wake kuhusu serikali za kali za utaifa barani Ulaya wakati wa kampeni zake za uchaguzi. Alitaja matukio yanayoendelea Belarus hadi Poland na Hungary na kuibuka kwa tawala za kimabavu ulimwenguni. Alisema mpinzani wake Rais Donald Trump anawaunga mkono wahuni wote ulimwenguni. Akimaanisha Rais Alexander Lukashenko wa Belarus, Andrzej Duda wa Poland na Waziri Mkuu wa Hungary Viktor Orban.

Soma zaidi: Maoni: Matarajio ya Afrika kwa Marekani

Mjini Warsaw, serikali ilionyesha diplomasia Zaidi na kumpongeza Biden kwa kile ilisema kampeni yenye mafanikio ya urais. Duda aliandika kwenye Twitter kuwa Poland imedhamiria kudumisha ushirikiano wa ngazi ya juu na ubora wa juu na Marekani kwa kuwa na muungano imara hata Zaidi. Rais wa Poland alikuwa na uhusiano wa kibinafasi na Trump n ahata akatiumia ziara ya White House kuipiga jeki kampeni yake.

Pongezi kutoka Budapest zilionekana kuwa za mseto. Mkuu wa ofisi ya waziri mkuu Viktor Orban, Gergely Gulyas alisema alikuwa na mashaka wakati wa kuhesabiwa kura kote Marekani. Anasema anatumai sera ya kigeni ya serikali mpya ya chama cha Democratic itakuwa bora kuliko iliyopita, akimaanisha utawala wa Obama ambao Biden alihudumu kama makamu wa rais.

Peter Kreko kutoka shirika la Taasisi ya kiliberali ya Political Capital yenye makao yake mjini Budapest amesema urais wa Trump ulimaanisha kuwa msaada usio na masharti kutoka Washington. Sasa utawala wa Joe Biden utakuwa mkali sana kwa Hungary, kuhusu kushuka kwa demokrasia, na ufisadi unaohusiana na uwekezaji wa China na Urusi, mambo yaliyofumbiwa macho na Trump.

'Pigo kwa Kaczynski'

Poland ilikuwa nchi pekee ya Umoja wa Ulaya ambayo raia wengi walikuwa na mtazamo chanya kuhusu Trump, kwa mujibu wa tafiti zilizofanywa. Na ni kwa sababu Trump aliiunga mkono Poland katika ugomvi wake wa kijeshi na Urusi. Trump pia alikuwa mkosoaji mkubwa wa mradi wa bomba la gesi la Nord Stream 2, na akaunga mkono Mradi wa Bahari Tatu unaoongozwa na Poland.

Piotr Buras kutoka ofisi ya Mahusiano ya Kigeni ya Baraza la Ulaya anasema matokeo ya uchaguzi wa Marekani ni pigo kwa Kaczynski na Orban, kwa sababu wote wamuewekea dau Trump.

Soma zaidi: Maoni: Rais mpya - lakini hakuna mshindi

Kwa mujibu wa Buras, chini ya Biden hali itabatilishwa: Poland itapendeza tu kama mshirika kama itaendeleza uhusiano mzuri na Ujerumani. Na amesema Biden ataimarisha na sio kudhoofisha Umoja wa Ulaya na bila shaka hataki Ujerumani kutengwa.

Marcin Zaborowski, mwanahabari wa jarida la Res Publica Nova, pia alisema serikali ya Poland imempoteza mshirika wake wa karibu wa kiitikadi. Amesema chama tawala cha PiS kitayachukulia mabadiliko ya utawala Marekani kwa wasiwasi kama sio kwa uhasama wa wazi.

Kurejea kwa hali ya kawaida?

Sergey Lagodinsky, Mjerumani wa chama cha Kijani katika Bunge la Ulaya, amesema anadhani itakuwa bora kwa Umoja wa Ulaya wakati kutokuwepo kwa Trump hakutaweza tena kuziimarisha serikali za siasa kali za utaifa barani Ulaya. Amesema Biden atakuza ushirikiano wa Umoja wa Ulaya na sio kujaribu kutafuta upendeleo wa serikali binafsi.

Soma pia: Maoni: Uchaguzi Marekani - Trump ahujumu demokrasia

Lagodinsky anasema kushindwa kwa Trump ni pigo kwa serikali za utaifa kote duniani, lakini pia akaonya dhidi ya kutangaza ushindi. Anaongeza kuwa bila rais wa Marekani mwenye nia ya kuugawa na kuudhoofisha Umoja wa Ulaya, maisha ya kisiasa katika Umoja wa Ulaya huenda kwa kiasi Fulani yakarejea katika hali ya kawaida.

Bruce Amani
https://www.dw.com/en/with-donald-trump-out-eu-nationalists-are-down-a-us-ally/a-55559084