Mzozo wa uchumi hasa upo nchi zinazoendelea
5 Oktoba 2009Mwanzoni hiyo wala haieleweki vizuri, kwani mzozo wa uchumi na fedha unaendelea kuathiri nchi nyingi zingine duniani na ni tatizo kubwa sana, hasa katika nchi zinazoendelea. Nchi hizo zimepungukiwa uwekezaji wa moja kwa moja, mapato ya mauzo na mitaji yake inaendelea kupunguka. Hiyo ni mitaji iliyodhaminiwa kwa misaada ya nchi tajiri zilizoendelea kiviwanda. Matukio kama hayo bila shaka yatasababisha matatizo makubwa zaidi ya malipo katika nchi masikini. Kwa hivyo nchi hizo zitaendelea kutegemea Shirika la Fedha la Kimataifa IMF na kuwa wateja wa kudumu wa Benki ya Dunia.
Ikiwa huo ni ukweli wa mambo, basi kwa nini wataalamu,mawaziri wa fedha na magavana wa benki wanaokutana mjini Istanbul wanashauri kuachana na mipango iliyowekwa kudhibiti mzozo wa kiuchumi duniani? Jawabu ni somo lililopatikana kwa sehemu fulani kutokana na mzozo wa fedha wa hivi karibuni. Hasa watalamu wameona kuwa mbali na kutokuwepo kwa uwiano wa kibiashara, matumizi makubwa ya Marekani kufuatia mashambulizi ya kigaidi ya Septemba 11, ni chanzo cha mzozo wa mikopo ya nyumba ambao hatimae ulisababisha mgogoro wa kiuchumi kila pembe ya dunia.
Ilikuwa sahihi kutumia pesa ili kuzuia uchumi kudorora kote duniani,lakini ilikuwa kosa kusahau kuivuta kamba kwa wakati. Kwa maneno mengine, mtu akikosa kujitoa kwa wakati basi hupanda mbegu ya mzozo mpya. Hata mashirika ya fedha ya kimataifa yanapaswa kutambua ukweli huo.
Lakini, Mkurugenzi Mkuu wa IMF Dominique Strauß-Kahn hachoki kuionya jumuiya ya kimataifa kutotangaza mapema sana kuwa mgogoro wa kiuchumi umeshadhibitiwa. Hiyo ni sawa, lakini ni dhahiri kuwa sehemu ya mkakati wake ni kuendelea na huduma za IMF na kuhalalisha mtaji wa shirika hilo. Lakini kuna wakati ambapo hata IMF hupaswa kuvuta kamba kwani mikopo mingi huenda ikasababisha madhara makubwa.
Kwa upande mwingine, Benki ya Dunia iliyo na wajibu wa kupiga vita umasikini ni tofauti. Mtaji wake ni kama dola bilioni 100 tu kinyume na bilioni 500 zilizokusanywa katika IMF. Hiyo ni ishara kuwa vita dhidi ya umasikini si mada inayopewa kipaumbele hivi sasa katika nchi za magharibi. Ni ishara mbaya sana. Kwani mzozo wa kweli bado upo njiani na utatokea katika nchi zinazoendelea barani Afrika. Wasababishaji wa hali hiyo wapo Ulaya lakini watakaoathirika vibaya ni masikini wanaoishi kwengineko. Kwani nchi zinazoendelea hazina njia nyingine ila kuchukua mikopo ili ziweze kupambana na mizozo iliyosababishwa na wengine. Na hapo tena kuna hatari ya mikopo mipya kuanza kurundikana.
Mwandishi: Wenkel,Rolf /ZPR
Mhariri:M.Abdul-Rahman