1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mwakilishi Maalum wa katibu mkuu wa UN afanya ziara DRC

Mitima Delachance10 Machi 2021

Mwakilishi maalum wa katibu mkuu wa umoja wa mataifa nchini jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, Bintou Keita amefanya ziara ya siku moja mjini Bukavu hii leo.

https://p.dw.com/p/3qRmY
DR Kongo Treffen Bintou Keita und Félix Tshisekedi
Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Bintou KeitaPicha: Giscard Kusema/Kommunikationsdienst DR Kongo

Lengo la ziara hiyo ni kujionea hali ya mambo na kujadili masuala ya usalama pamoja na viongozi wa mikoa ya mashariki ya jamhuri ya kidemokrasia ya Congo.

Ziara hii ya kwanza ya Bintou Keita, ilianzia jana mjini Goma katika mkoa wa Kivu ya Kaskazini ambapo alizungumza na Gavana wa mkoa huo Carly Nzanzu Kasivita kuhusu hali ya ukosefu wa usalama mashariki ya jamhuri ya kidemokrasia ya Congo kwa ujumla na hususan katika mikoa ya kivu ya kaskazini na kivu ya kusini, ambapo kuna ripotiwa mashambulizi dhidi ya baadhi ya vijiji kila mara katika maeneo ya Beni huko kivu kaskazini na mitaa ya Uvira na Fizi hapa kivu kusini.

Alipokutana na kaimu gavana  wa mkoa wa kivu kusini Marc Malago Kashekere, Bintou Keita ambaye pia ni mkuu wa Ujumbe wa Amani wa Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, MONUSCO,  alihakikisha nia ya umoja wa mataifa kushirikiana na serikali ya jamhuri ya kidemokrasia ya Congo katika juhudi zake za kuleta amani na usalama katika mikoa ya mashariki.

Bintou Keita amesema: "Changamoto za kiusalama, uwepo wa makundi yenye silaha katika mashariki ya Congo ni shida kabisa. Lakini suluhisho litafikiwa kwamba mamlaka ya kitaifa na jamii, zitashiriki katika kutafuta suluhisho na kwa kupokonya silaha makundi hayo kwa kupunguza nguvu zao na kujumuisha tena wapiganaji wazamani katika jamii hadi kufikia utulivu. Hivyo ni vipaumbele vikuu”

Kumekuwa na ongezeko la visa vya ukosefu wa usalama 

DRK Nach Überfall auf Konvoi von Luca Attanasio
Picha: Justin Kabumba/AP/dpa/picture alliance


Ziara hii ya Bintou Keita mjini Bukavu inafanyika wakati huu ambapo asasi za kiraia katika mkoa wa kivu kusini zinatoa malalamiko kuhusu ongezeko la hali ya ukosefu wa usalama kutokana na uwepo wa makundi yenye kumiliki silaha yanayoundwa na vijana raia wa jamhuri ya kidemokrasia ya Congo napia makundi kutoka nchi jirani za Rwanda na Burundi yanayojificha katika misitu ya kivu kusini kwa miongo kadhaa. Kitandala Santos ni kiongozi wa shirika la raia wa wilaya ya Fizi.

Anakosoa Monusco kwavile imebakilia kufanya uchunguzi bila kuingilia kati kurejesha usalama kama ilivyo tarajiwa na raia wa Congo. Lakini kiongozi wa Monusco Bintou Keita ameonya kwamba licha ya mapungufu, kuna pia mafanikio mazuri ambayo Monusco ilileta katika sekta tofauti:

"Kipaumbele cha kwanza kulingana na agizo la Monusco ni ulinzi wa raia. Kile ningependa ni kwamba tuzungumze pia juu ya juhudi zinazofanywa na Monusco kulinda raia. Sio kinga ya mwili tu. Kuna vitengo mbalimbali vya Monusco ambavyo vinafanya kazi katika sekta kadhaa kwa mfano kuboresha umoja na mshikamano wa kijamii, uboreshaji wa kufikia haki”


Magavana wa kivu ya kaskazini na kivu kusini wameonesha nia ya kuimarishwa kwa mfumo wa usalama wa Congo kupitia mchango wa umoja wa mataifa ambao tangu muda kitambo umeanza kujadili mpango wa kujiondoa nchini Congo.