1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiAsia

Mtanzania aliyeuawa vitani Urusi arudishwa nyumbani kuzikwa

Mohammed Khelef
27 Januari 2023

Mwili wa raia wa Kitanzania, Nemes Tarimo, aliyeuawa vitani nchini Urusi mwezi Oktoba 2022, umewasili nchini Tanzania saa 12:00 asubuhi ya leo katika uwanja wa ndege wa kimataifa Mwalimu Julius Kambarae Nyerere.

https://p.dw.com/p/4MmI1
Ukraine Krieg l Ukrainische Artillerie, Haubitze M-777 nahe Kherson
Picha: Metin Aktas/AA/picture alliance

Mara tu baada ya ndege kutua katika uwanja wa ndege jijini Dar es Salaa, ndugu, jamaa na marafiki, ambao walikuwa wanasubiri kuupokoea mwili wa mpendwa wao, waliangua vilio huku jeneza likiwekwa kwenye gari.

Msafara wa mwili wa marehemu, ulielekea Mbezi kwa Msuguri nyumbani kwa dada yake, Salome Kisare.                                                                                                                                                                                                                                        Kwa upande wake, baba mdogo wa Nemes, Dickson Muro, alisema Nemes aliwapigia simu kuwa amepata matatizo na ameshtakiwa polisi, lakini pindi walipoanza kutafuta mwanasheria, aliwaambia waache kwa kuwa angelipambana mwenyewe.

Kwa mujibu wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Stagomerna Tax, Nemes  Tarimo alikwenda Urusi na kujiunga na Chuo Kikuu cha jijini Moscow  kifahamikacho kama MIREA mwaka 2020 kwa masomo ya shahada ya uzamili katika fani ya  biashara, lakini miaka miwili baadaye alihukumiwa kifungo cha miaka saba nchini humo kwa madai ya vitendo vya uhalifu.

Waziri huyo amesema wizara yake imepokea taarifa kutoka serikali ya Urusi kuwa akiwa gerezani, Tarimo alipewa nafasi ya kujiunga na kikundi cha kijeshi cha Urusi kiitwacho Wagner kwa ahadi ya kulipwa fedha na kuachiwa huru baada ya kumalizika kwa vita hiyo.

Imeandikwa na Florence Majani, DW Dar es Salaam