1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa NATO- Strasbourg

3 Aprili 2009

Jumuiya ya NATO bado ni nguzo muhimu ya usalama wa Marekani. Ni matamshi ya Rais Barack Obama, anayehudhuria mkutano wake wa kwanza wa NATO.

https://p.dw.com/p/HPiZ
Rais Nicholas Sarkozy na Barack Obama.Picha: AP


Angela Merkel - NATO-Rede
Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel.Picha: AP

Katika maadhimisho hayo ya miaka 60 tangu NATO kuasisiwa, Obama alitoa mwito wa kuwepo kwa Ulaya yenye nguvu. Baada ya mkutano na Obama, rais Nicholas Sarkozy alisema Ufaransa imekubali itamchukua mahabusu mmoja kutoka jela la Guantanamo ambalo litafungwa.

'' Tunataka washirika wa dhati.....tunataka kuona Ulaya iliyo na ulinzi imara. Ndio ujumbe alikuwa nao Barack Obama baada ya mkutano na rais wa Ufaransa Nicholas Sarkozy, mjini Strasbourg......saa kadhaa kabla ya kuanza kwa mkutano wa jumuiya ya NATO.


Baden Baden vor dem Nato Gipfel
Polisi washika doria, kabla ya mkutano wa NATO mjini Baden Baden Ujerumani.Picha: AP

Obama alisema jumuiya ya NATO ambayo inaadhimisha miaka 60 tangu ilipoasisiwa ni nguzo muhimu katika ulinzi wa Marekani na Ulaya kwa jumla. Lakini la muhimu kabisa ni mwito wa Obama kwa nchi za bara ulaya. Obama akasema matumaini yake ni kutilia nguvu ushirikiano na uhusiano wa Marekani na Ulaya. Marekani ina matumaini katika mkutano huu wa NATO itashawishi nchi zingine kuchangia wanajeshi nchini Afghanistan. Swala litakalokuwa katika ajenda katika mkutano huu wa NATO.



'' Hatuwezi kufikia lengo hili pekee yetu.....kama ilivyokuwa siku za nyuma wakati wa vita vya pili vya dunia, lazima tushirikiane na tunajua mageuzi ni kitu kinachowezekana kwa pande zote, kwa kila kitu tunachotofautiana kuna mitazamo inayotuunganisha na kuonyesha sisi sote tuko sawa.'' Alisema Obama


Kwa upande wake Nicholas Sarkozy alisema yuko tayari kushirikiana na Rais Obama, katika masuala mengi ikiwemo Afghanistan. Na hasa Sarkozy alimpongeza Obama kwa kufunga jela la Guantanamo. Kulingana na Sarkozy jela la Guantanamo liilidhalilisha maadili ya Marekani kuhusiana na masuala ya haki za kibinadamu.


Sarkozy akatangaza kuwa Ufaransa imekubali kumchukua mahabusu mmoja kutoka jela la Guantanamo liitakalofungwa hivi karibuni. Mahabusu huyo anasemekana ni raia wa Algeria. Ufaransa na Algeria zina uhusiano wa kihistoria. Sarkozy pia akapokea mwito wa Obama wa inahitaji washirika wa dhati, wala si wadhaifu.



'' Rais Obama hanihitaji ili kuelewa kwamba ulaya yenye nguvu, ulaya ya ulinzi iliyopo ni jaza kwa Marekani. Marekani inayoongozwa na rais Obama haitaki washirika dahifu, inahitaji watu imara na wanaobeba dhamana zao.'' Akasema Sarkozy


Ufaransa itarejea upya kuwa mwanachama kamili wa jumuia ya kujihami ya NATO,kesho jumamosi,miaka 43 baada ya Charles de Gaule kuitoa nchi yake katika uongozi wa kimkakati wa kijeshi na kuamuru vituo vyote vya kijeshi vya Marekani vifungwe nchini Ufaransa.


Katika wakati ambapo viongozi wa NATO wanakutana,vikosi vya polisi vinaendelea kuimarisha usalama kuzuia machafuko yeyote. Hii ni baada ya watu 300 kutiwa nguvuni katika makabiliano ya polisi na waandamanaji.


Mkutano huu wa NATO wa siku mbili unaondaliwa na Ujerumani na Ufaransa, unakusudiwa kujadili masuala mengi, lakini yatakayopewa kipao mbele ni hali nchini Afghanistan, uhusiano wa mvutano kati ya Jumuiya hii ya NATO na Urusi.


Baadaye Obama atakutana pia na Kansala wa Ujerumani Angela Merkel. Shughuli rasmi ya mkutano wa NATO zitaanza baadaye leo jioni. Mji wa Strasbourg, Ufarsana na Baden Baden Ujerumani ndio wenyeji shirika wa mkutano huu.


Mbali na Ufaransa kujiunga upya, NATO pia itakuwa inakaribisha washirika wapya Albania na Croatia.


Mwandishi: Munira Muhammad/ AFP

Mhariri: Mohammed Abdulrahaman