1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkutano wa kimataifa kuhusu uhai anuai

18 Oktoba 2010

Mkutano wa nchi zilizotia saini mkataba wa uhai anuai (CBD) umefunguliwa hii leo katika mji wa Japan,Nagoya kwa azma ya kuendeleza mikakati ya kupunguza kasi ya kutoweka kwa mimea na kuteketezwa kwa mazingira.

https://p.dw.com/p/Ph5J
Ahmed Djoghlaf, Executive Secretary of the Convention of Biological Diversity (CBD) gestures during his opening ceremony speech of the tenth meeting of the Conference of the Parties to the Convention on Biological Diversity (CBD COP 10) in Nagoya city, Aichi prefecture, Japan, 18 October, 2010. Representatives of over 190 signatories to a United Nations biodiversity pact gather for the two-week conference. EPA/EVERETT KENNEDY BROWN +++(c) dpa - Bildfunk+++
Ahmed Djoghlaf, Katibu Mtendaji wa CBD akizungumza katika ufunguzi wa mkutano wa 10 wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhai anuai mjini Nagoya,Japan.Picha: picture alliance/dpa

Kwenye mkutano huo wa 10 wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhai anuai, utakaodumu majuma mawili, wajumbe kutoka nchi 193 watajadiliana pia njia ya kugawana faida za raslimali za urithi wa kibiolojia. Lakini nchi tajiri na zile zinazoendelea zinatofautiana katika masuala muhimu. Kwa hivyo kuna wasiwasi kwamba tofauti hizo huenda zikakwamisha majadiliano yao kama ilivyotokea katika mikutano ya mabadiliko ya tabia nchi. Vile vile wajumbe kwenye mkutano huo wa nchi zilizotia saini mkataba wa uhai anuai wanasema, itakuwa vigumu kuweka malengo kuhusu njia za kuhifadhi ardhi na bahari za dunia kwa sababu ya tofauti hizo.

Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, chini ya asilimia 1 ya bahari na kama asilimia 12 ya ardhi ndio inayolindwa. Lakini maeneo yanayolindwa na kutunzwa vizuri husaidia kuendeleza mifumo ya kiekolojia. Hayo yote husaidia afya ya binadamu. Maeneo kama hayo yangeweza kuwa kama kinga dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi na umasikini.

Kwa hivyo ni muhimu kwa mataifa hayo kuongeza sehemu ya maeneo yanayohifadhiwa. Kwa mfano, asilimia 15 ya bahari na asilimia 25 ya ardhi duniani ziwe chini ya ulinzi. Lakini jitahada kama hizo bila shaka zitapingwa vikali na makundi ya wafanya biashara.

Mkataba wa uhai anuai uliotiwa saini mwaka 1992 wakati wa mkutano wa mazingira wa Rio de Janeiro nchini Brazil, kama mkataba wa Umoja wa Mataifa juu ya mabadiliko ya tabia nchi. Mkataba huo wa uhai anuai umeweka malengo matatu makuu: kuhifadhi uhai anuai: kutumia uhai anuai kwa njia endelevu na kugawana faida za raslimali za urithi wa kibiolojia kwa haki na usawa. Mwaka 2002 nchi zilizotia saini mkataba huo ziliahidi kupunguza kwa kiwango kikubwa kasi ya uharibifu wa uhai anuai ifikapo mwaka 2010 na kupunguza umasikini na kunufaisha maisha. Lakini malengo hayo hayakutimizwa.

Majadiliano ya ngazi za juu yamepangwa kufanywa Oktoba 27 hadi 29, ikitazamiwa kuwa mawaziri watakaohudhuria mkutano huo watafanikiwa kupata makubaliano yatakayokamilisha majadiliano ya uhai anuai.

Mhariri: Martin,Prema/DPAE/APE

Mpitiaji: M.Abdul-Rahman