1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Seneta Hillary Clinton amwuunga mkono Obama.

Mtullya, Abdu Said27 Agosti 2008

Seneta Hillary Clinton asema lazima chama cha Demokratik kisimame pamoja ili kumwuunga mkono Barack Obama.

https://p.dw.com/p/F5Tl
Seneta Hillary Clinton akihutubia kwenye mkutano mkuu wa chama cha Demokratik mjini Denver.Picha: Rocky Mountain News, Ken Papaleo

Seneta wa  jimbo  la  New York  Hillary Clinton ametoa mwito kwa  wafuasi wake wote wamwuunge mkono seneta Barack Obama  anaegombea urais wa Marekani  kwa tiketi ya chama cha Demokratik.

Seneta Clinton ametoa mwito huo katika siku ya pili ya  mkutano mkuu wa chama hicho unaofanyika  mjini  Denver, Colorado.

Seneta  Clinton  amewataka  wafuasi wake  wasimame  pamoja  ili wamwezeshe Barack Obama kuingia Ikulu ya Marekani  kama  rais.

Hillary Clinton alieshindwa  na Obama katika kugombea nafasi  ya kukiwakilisha chama cha demokratik ,amesema sasa wakati umefika kwa  wote  kusimama kama chama kimoja. Aliwaambia wajumbe  zaidi ya alfu nne wanaohudhuria  mkutano mkuu  wa chama hicho, kuwa Obama ni mjumbe wake na lazima awe  rais . Huku akishangiliwa kwa mayowe  ya  furaha , seneta huyo wa jimbo la New York aliendelea kusema asilani ,abadan, hakuna  cha  MacCain.

Amesema hakutumia miaka  35 iliyopita katika  mahandaki  kutetea haki za watoto, kuendesha kampeni  ili wamarekani wote  wapate huduma  za afya, na wala hakutumia miaka hiyo kuwasaidia  wazazi, familia, na kutetea haki  za  akina  mama nchini Marekani na duniani  kote, halafu kuja kumwona mtu mwengine  wa chama  cha Republican  akiingia  katika Ikulu. "Hapana"

Amewataka wamerekani wote milioni 18 waliompigia  kura katika uchaguzi wa kutafuta  mjumbe  wa  kukiwakilisha chama  cha demokratik kugombea urais, sasa wasimame pamoja na Obama.

Amesema  wote  sasa wamo katika timu moja, na  hakuna anaeweza  kusimama kando katika  mapambano  ya  kutetea mustakabal wa Marekani.

Ametamka kuwa lazima chama cha demokratik  kishinde katika mapambano hayo.


Akiwahutubia wajumbe kwenye mkutano huo aliekuwa gavana wa jimbo la Virginia Mark Warner  amesema kuwa seneta  Obama ndiye mtu atakeifaa Marekani. Amesema  uchaguzi wa rais nchini Marekani  safari hii ni mashindano  ya  kupigania  mustakabal wa  nchi.

Gavana  huyo wa zamani ameeleza kuwa Marekani haitaweza kuzikabili changamoto za ushindani  za  karne ya 21 ikiwa itaongozwa na rais alienaswa katika  zama zilizopita.

Gavana huyo  wa zamani Warner pia ameulaumu  utawala wa rais Bush kwa kutumia sera potovu  na  itikadi  za kizamani katika  uongozi  wake.   

Wajumbe kwenye mkutano  mkuu wa siku nne wa   chama  cha  demokratik wanatarajiwa kumpitisha   rasmi seneta Barack Obama kugombea urais wa Marekani mnamo   mwezi novemba.