1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkataba mpya wa ulaya watiwa saini Lisbonne

Oummilkheir13 Desemba 2007

Umoja wa ulaya wajipatia mkataba mpya utakaorahisisha shughuli za taasisi zake

https://p.dw.com/p/CbJS
Kansela Angela Merkel ,waziri wa nje Steinmeier katika sherehe za kutia saini waraka mpya mjini LisbonnePicha: picture-alliance/ dpa

Viongozi 27 wa taifa na serikali wa Umoja wa ulaya,au wawakilishi wao walikusanyika hii leo mjini Lisbonne nchini Ureno katika sherehe za kutia saini mkataba uliofanyiwa marekebisho,unaoshika nafasi ya katiba iliyokataliwa ya Umoja wa Ulaya.Mkataba huo mpya ulengwa kurahisisha shughuli za Umoja mpana wa Ulaya.

Waziri mkuu wa Ureno José Socrates amewakaribisha viongozi wa taifa na serikali katika jumba la fakhari la ibada-HIERONYMUS kulikofanyika sherehe za kutia saini waraka mpya unaojulikana kama “Mkataba wa Lisbonne”.Kila kiongozi wa taifa na serikali alipewa kalamu ya fedha yenye jina lake ili kuweka saini yake katika mkataba huo.

Waziri mkuu wa Uengereza Gordon Brown ,hakushiriki katika sherehe hizo,badala yaker amewakilishwa na waziri wake wa mambo ya nchi za nje David Miliband.Hata hivyo kiongozi huyo wa serikali ya uengereza amepangiwa kuwasili Lisbonn baadae kuhudhuria karamu maalum iliyoandaliwa na kutia saini pia waraka huo.

Viongozi mmoja mmoja wamekwenda kuweka saini yao katika waraka huo uliopitishwa October 19 iliyopita katika mji mkuu wa Ureno na kushika nafasi ya katiba ya umoja wa ulaya iliyokataliwa mwaka 2005 kwa kura ya maoni nchini Ufaransa na Uholanzi.

Ilikua Ujerumani, ilipokua mwenyekiti wa zamu wa Umoja wa Ulaya,mnamo nusu ya kwanza ya mwaka huu iliyotia njiani waraka huo uliofanyiwa mageuzi,mwezi June uliopita.

Kabla ya kuweka saini yake kansela Angela Merkel wa Ujerumani alisema:

“Tunafurahi bila ya shaka sio tuu kushiriki bali pia kuweza kusema kwamba serikali kuu ya Ujerumani imechangia pia katika kufanikisha mkataba huu.Leo ni siku muhimu kwa ulaya na inafungua njia kwa nchi zote kuidhinisha mkataba huu.Na ndio maana,nnaamini,mkataba huu ukianza kufanya kazi,Ulaya itakua imefungua ukurasa mpya.”

Mkataba huu mpya uliofanyiwa marekebisho,ukiidhinishwa na nchi zote 27 wanachama wa umoja wa ulaya,unatarajiwa kuanza kufanya kazi January mosi mwaka 2009.

Nchi nyingi,isipokua Ireland,inayolazimika kuitisha kura ya maoni ya wananchi,zimeshatangaza azma ya kuidhinisha mkataba huo bungeni-wakihofia kishindo kilichotokana na kura ya La ya Ufaransa na Uholnazi miaka miwili na nusu iliyopita.

Licha ya msimamo huo,shinikizo la wanaotaka wananchi waulizwe maoni yao linazodi kupata nguvu.Jana azimio la haki za kimsingi lilipopitishwa katika bunge la Ulaya,sauti zilipazwa na baadhi ya wabunge wanaoshikilia wananchi waulizwe maoni yao kama wanaunga mkono au la mkataba huo.

Baada ya sherehe za leo mjini Lisbonne za kutia saini mkataba mpya wa umoja wa ulaya,na karamu iliyoandaliwa kwaajili hiyo,viongozi wa taifa na serikali wa Umoja wa ulaya watakutana tena kesho asubuhi mjini Brussels kwa kikao chao cha mwisho wa mwaka-kitakachokamilisha pia zamu ya Ureno kama mwenyekiti wa umoja wa ulaya.