1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mionzi ya Nyuklia yasambaa ndani na nje ya Japan

Saumu Ramadhani Yusuf29 Machi 2011

Kiwango kidogo cha mionzi inayovuja katika kinu cha Nyuklia cha Fukushima kimesambaa

https://p.dw.com/p/10jdQ
Mionzi ya Nyuklia yazagaa JapanPicha: Tepco/Kyodo/AP/dapd

Serikali za China,Korea Kusini,Ufilipino na Vietnam zimeripoti kwamba mionzi ya Nyuklia imeshaingia katika nchi zao ingawa serikali hizo zimesisitiza kwamba  viwango vilivyogunduliwa ni vodogo  na haviwezi kusababisha madhara ya kiafya.Msemaji katika taasisi ya utafiti wa masuala ya Nyuklia ya Ufilipino Tina Cerbolis akiunga mkono taarifa zilizotolewa na maafisa wa nchi hizo nyingine za Asia amesema kuna kiwango kidogo cha mionzi iliyogunduliwa kwenye hewa katika nchi hizo.

Hata hivyo hali hiyo inaendelea kuwapa wasiwasi  watu wa eneo hilo la Asia.Kusambaa huko kwa mionzi ni athari inayotokana na kuharibiwa kwa kiwanda cha Nyuklia cha Fukushima zaidi ya wiki mbili baada ya kutokea tetemeko kubwa la ardhi lililosababisha janga la Tsunami.Aidha inaarifiwa kwamba mionzi hiyo imegunduliwa hadi nchini Marekani ambapo maji ya mvua katika eneo la Ohio yamegundulika kuathirika.

Maafisa wanaohusika na masuala ya Mazingira nchini Marekani wamesema kwamba mionzi katika maji ya Mvua huko Ohio imegunduliwa hapo jana jumatatu.Watu pamoja na nchi zilizoko karibu na Japan tayari zimeshachukua hatua kadhaa za tahadhari wakati mgogoro huo ukitapakaa.Serikali nyingi katika eneo hilo zimeshaanza shughuli za kuvivanyia utafiti wa Mionzi vyakula vinavyoagizwa kutoka Japan wakati mboga zinazokuzwa karibu na eneo la viwanda la Fukushima zimepigwa marufuku kusafirishwa nje ya eneo hilo.

Wasafiri wanaotokea nchini  Japan pia wameshaanza kufanyiwa uchunguzi katika baadhi ya viwanja vya ndege.Nchini China  watu wawili waliotokea nchini  Japan walilazwa hospitali wiki iliyopita  baada ya maafisa wa uwanja wa ndege  kuwagundua na kiwango cha juu cha mionzi ingawa baadae watu hao waliruhusiwa kuondoka Hospitali.

Baraza la linaloshughulikia masuala ya Atomiki huko katika kisiwa cha Taiwan  limesema hii leo kwamba kiwango kidogo cha mionzi kimegunduliwa kwa wasarifi 43 kutoka Japan tangu mzozo huo wa Nyuklia ulipozuka .Aidha sekta ya usafiri wa meli imeingiwa na wasiwasi mkubwa kuhusiana na uwezekano mkubwa wa meli zinazosari katika Bahari ya  pwani ya Japan ambayo imeshaathirika na mionzi  kusambaza mionzi hiyo kwa kasi.

Maafisa wa China wiki iliyopita wamesema kwamba mionzi pia imegunduliwa katika mezi za mizigo  kutoka Japan katika bandari ya kusini mashariki ya mji wa Xiamen.Aidha hii leo kitisho kimeongezeka zaidi kwamba kuna uwezekano mkubwa sana wa mionzi hiyo kuendelea kusambaa katika eneo hilo.Maafisa wa Korea Kusini wamesema wameanza kuwachunguza samaki wanaovuliwa katika pwani ya nchi hiyo.

Mwandishi :Saumu Mwasimba/ AFPE

Mhariri :Abdul-Rahman ,Mohammed