1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel, Schulz wakamilishia kampeni nyumbani

Iddi Ssessanga
23 Septemba 2017

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na mpinzani wake mkuu Martin schulz wamerejea katika majimbo yao ya nyumbani kuhitimisha kampeni kabla ya uchauguzi wa Jumapili, wakiwahimiza Wajerumani kukikataa chama cha AfD.

https://p.dw.com/p/2kZ6l
Deutschland Plakate Bundestagswahlen 2017
Picha: Getty Images/S. Gallup

Merkel atakamilisha ratiba ya kampeni yake katika jimbo lake la Merklenburg - Vorpommern lililoko katika pwani ya Baltic siku ya Jumamosi.

Lakini mbali na kuongoza wilaya ambako chama cha chake cha Christian Democratic Unioni kinaungwa mkono zaidi, atazitembelea pia wilaya za mji wa Greifswald na kisiwa cha Ruegen ambako chama kinachouchukia Uislamu cha Alternatuve für Deutschland - Chama Mabadala kwa Ujerumani - kilipata mafanikio makubwa katika uchaguzi wa jimbo mwaka uliopita.

Msosho demokratik Martin Schulz anakamilishia kampeni zake Aachen, mji wa Magharibi mwa Ujerumani ulioko jirani na mji wake wa kuzaliwa wa Wuerselen.

Wasiwasi watawala kuhusu AfD

Ingawa chama cha Merkel kina uongozi wa tarakimu mbili kulingana na uchunguzi wa maoni dhidi ya chama cha Social Democratic SPD, kinachoshika nafasi ya pili, wasiwasi unazidi miongoni mwa vyama vikuu kutokana na maoni ya hivi karibuni ya wapigakura kuonyesha uungwaji mkono wa chama cha AfD ukiongezeka katika muda wa mwisho wa kampeni kwa kati ya asilimia 11 na 13.

Deutschland AfD-Pressekonferenz mit Weidel und Gauland
Wagombea wakuu wa chama cha AfD, Alexander Gauland (kulia) na Alice Weidel.Picha: Reuters/A. Schmidt

Hiyo inamaanisha kwamba wawakilishi 60 wa chama hicho kinachopinga waziwazi uhamiaji huenda wakaingia katika bunge la Ujerumani - Bundestag kwa mara ya kwanza tangu kumalizika kwa vita kuu vya pili vya Dunia, jambo linalovisukuma vya vikongwe kuwashawishi wapigakura wakitenge chama hicho kichanga.

Wakati wa hotuba kubwa ya mwisho ya Merkel siku ya Ijumaa jioni katika mji wa kusini wa Munich, wapinzani walipiga firimbi na kupuliza vuvuzela huku wakiimba nyimbo za kumtaka aondoke. Lakini kiongozi huyo mwenye umri wa miaka 63 alisimama kidete na kuendelea na hotuba yake, akiwaambia waliokuwa wanamsikiliza kwamba Ujerumani haitojengwa kupitia firimbi na wazomeaji.

Katika mwito wake kwa wapigakura kuungana na kukizuwia chama cha AfD, Schulz aliuambia mkutano katikati mwa mji wa Berlin kwamba "Chama Mbadala kwa Ujerumani siyo mbadala. Ni aibu kwa taifa letu."

Wanazi halisi bungeni

Waziri wa mambo ya kigeni Sigmar Gabriel, pia kutoka chama cha Sosho demokratik, alisema chama cha AfD kinaongozwa na watu wanaochochea chuki, wanaoeneza propaganda za Wanazi." "Kwa mara ya kwanza tangu vita kuu vya pili vya dunia, Wanazi halisi wataka katika bunge la Ujerumani," alisema Gabriel.

Kampeni za uchaguzi huu zilizodumu kwa miezi miwili hazikuwa na msisimko mkubwa sana, ambapo wagombea wakuu wamekuwa wakitenganishwa na mambo machache motomoto. Wakati Merkel amekuwa akitetea agenda yake ya utulivu na mafanikio, na Schulz akitafuta kuwashawishi wapigakura kwa ahadi yake ya usawa zaidi wa kijamii, AfD imehamisha nadhari.

Mwandishi makala wa gazeti la Sueddeutsche Heribert Pranti, alimsifu kansela siyo tu kwa kuendelea na mikutano yake licha ya upinzani kutoka kwa wafuasiwa AfD, lakini pia kwa kuwalaani waziwazi wafuasi hao wa siasa kali za kizalendo za mrengo wa kulia.

Deutschland | Bundestagswahl 2017 | Wahlplakat CDU
Mabango ya wagombea wakuu, kansela Angela Merkel na Martin Schulz yakipamba barabara katika maeneo mbalimbali ya Ujerumani.Picha: picture-alliance/R. Goldmann

Miiko ya bunge kuvunjwa

Lakini mwandishi huyo alisikitika kwamba hilo limekuja kuchelewa katika kampeni "ilipodhihirika namna mazingira ya kisiasa yatakapobadilika wakati chama cha AfD kiko bungeni." "Siyo tu wanasiasa wa kizalendo, lakini pia wabaguzi na wenye imani kali wataingia bungeni," aliandika, na kuongeza kuwa "uzito wa hali hiyo ulitambuliwa kwa kuchelewa sana."

Thorsten Benner, mkurugenzi wa taasisi ya Sera ya umma ya dunia ya mjini Berlin, alisema AfD "itapinga masuala muhimu" bungeni, na kuonya kuwa miiko ya tangu 1945 inayoweza kuvunjwa ni pamoja na namna Ujerumani inavyoitazama historia yake ya Vita Kuu vya Pili vya Dunia, na suala la Mjerumani ni yupi.

Mmoja wa wagombea wakuu wa AfD, Alexander Gauland, aliwatolea mwito Wajerumani waache kutubia matendo yao ya wakati wa vita. Pia alizusha hasira aliposema kwamba Kimishna anaehusika na ushirikishwaji wa wageni katika jamii Aydan Ozoguz anapswa "kutupwa Anatolia", akimaanisha kuwa kamwe hatokuwa Mjerumani kutokana na asili yake ya Kituruki.

Mwandishi: Iddi Ssessanga/afpe

Mhariri: Isaac Gamba