1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel na Macron waonya kuhusu mzozo wa Ukraine

Bruce Amani
23 Desemba 2017

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na rais wa Ufaransa Emmanuel Macron wamehimiza pande zinazochangia ukiukaji wa mpango wa kusitisha mapigano mashariki mwa Ukraine kutekeleza haraka maamuzi waliyoyafikia

https://p.dw.com/p/2psVg
Emmanuel Macron und Angela Merkel in Brüssel
Picha: Reuters/L.Marin

Siku ya Jumatano, pande zinazozozana katika mzozo wa mashariki ya Ukraine, zilikubaliana kuhusu mpango wa kuweka chini silaha ambao utatekelezwa katika kipindi cha Krismasi na Mwaka Mpya. Maafisa wa Ukraine, waangalizi wa kiusalama na washirika wa kimataifa walionya kuwa uamuzi wa Urusi kujiondoa katika kundi la Urusi na Ukraine la kudhibiti usitishwaji vita huenda kukaongeza mapigano Mashariki mwa Ukraine.

Katika taarifa yao ya pamoja, Merkel na Macron wamesema hakuna njia mbadala kwa makubaliano ya Amani. Wamewataka maafisa wa Urusi kurudi katika jopo hilo la pamoja la udhibiti na uratibu wa usitishwaji vita. Urusi iliilaumu Ukraine kwa kuzuia kazi zao na kupunguza uwezo wao kufika katika maeneo ya vita.

Wakati huo huo, Moscow, Urusi imesema leo kuwa Marekani inahimiza kile imekitaja kuwa ni umwagikaji upya wa damu mashariki mwa Ukraine kufuatia uamuzi wake wa kuipa Ukraine silaha hatari zaidi.

Ostukraine OSZE
Mpango wa kusitisha mapigano Ukraine wavurugwaPicha: Getty Images/AFP/A. Filippov

Katika taarifa yenye maneno mazito, naibu waziri wa mambo ya nje wa Urusi Sergei Ryabkov, ameilaumu Marekani kwa kuvuka mstari na kuchochea machafuko Mashariki mwa Ukraine, eneo linalofahamika kama Donbass.

Ryabkov amesema silaha mpya za Marekani zinaweza kusababisha kuwepo kwa waathiriwa wapya miongoni mwa majirani zao. Naibu mwengine wa waziri wa mambo ya nje Grigory Karasin amesema hatua ya Marekani itahujumu juhudi za kutafuta suluhisho la kisiasa nchini Ukraine.

Wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilitangaza Ijumaa kwamba Marekani imeamua kuipa Ukraine silaha imara zaidi za ulinzi kama sehemu ya juhudi za kuisaidia Ukraine katika mipango yake ya muda mrefu ya kujiimarisha kiulinzi.

Silaha hizo mpya zinajumuisha vifaru vilivyoundwa Marekani vya kuzuia makombora. Ukraine imekuwa ikihitaji vifaru hivyo ili kuimarisha ulinzi wake dhidi ya vifaru ambavyo vimekuwa vikishambulia mashariki ya Ukraine wakati wa vita ambavyo vimesababisha vifo vya zaidi ya watu 10,000 tangu mwaka 2014. Awali, Marekani iliipa Ukraine msaada wa vifaa na mafunzo na pia imeruhusu makampuni binafsi kuiuzia Ukraine silaha ndogondogo kama bunduki. Maafisa walioeleza kuhusu mpango huo hawakuruhusiwa kuuzungumzia na hivyo walitaka wasitambulishwe majina. Ukraine inailaumu Urusi kwa kutuma vifaru. Marekani pia imedai Urusi inawapa silaha na mafunzo kando na kusaidia wanaotaka kujitenga.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA
Mhariri: John Juma