1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Schalke wataiweza Man City?

11 Machi 2019

Ligi ya vilabu bingwa barani Ulaya itarudia mechi zake wiki hii ambapo Jumanne timu ya Ujerumani Schalke 04 itakuwa inakwenda Manchester kupambana na Manchester City.

https://p.dw.com/p/3EnHI
Fußball Champions League FC Schalke 04 - Manchester City
Picha: Reuters/Action Images/M. Childs

Mechi ya mkumbo wa kwanza iliishia 3-2 City wakipata ushindi. Kocha wa Schalke Domenico Tedesco amepewa mechi mbili tu na uongozi wa klabu hiyo ili aonyeshe kweli iwapo anaistahili kazi hiyo, baada ya klabu hiyo kukumbwa na msururu wa matokeo mabovu.

Lakini Manchester City nao wana matatizo yao, wiki iliyopita shirikisho la soka Ulaya UEFA lilitangaza kwamba linaanzisha uchunguzi rasmi dhidi ya klabu hiyo kuhusiana na matumizi ya pesa kupita kiasi katika usajili wa wachezaji, jambo ambalo huenda likawafanya wapigwe marufuku ya kushiriki Champions League msimu ujao iwapo watapatikana na hatia. Kocha wa City Pep Guardiola lakini amesema hata wakapigwa marufuku, jina la klabu halitoharibika.

"Hapana hauezi kuharibika. Nafikiri klabu ilitoa taarifa na siwezi kuongezea. Klabu inakubali kuchunguzwa na tunatumaini uchunguzi huo utaisha haraka na uamuzi utolewe. Nilisema msimu uliopita kwamba ninaamini kwa kile kilichofanywa na klabu lakini natumai watayasuluhisha haraka waondoe mazingira haya," alisema Guardiola.

Jumatano Bayern Munich watakuwa wanapambana na Liverpool uwanjani Allianz Arena baada ya mechi ya duru ya kwanza kuisha sare ya kutofungana.

Mwandishi: Jacob SafariReuters/AFPE/DPAE

Mhariri: Gakuba Daniel