1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya kuunda serikali Ujerumani yakamilika

Zainab Aziz
12 Januari 2018

Viongozi wa vyama vya CDU/CSU na kile cha SPD vimekubaliana kuanzisha mazungumzo ya kuunda serikali baada ya kukesha usiku mzima wakijadiliana. Vyama vitafanya mkutano na waandishi wa habari kutoa taarifa zaidi.

https://p.dw.com/p/2qjLb
Deutschland Sondierungsgespräche in Berlin Merkel und Schulz
Picha: Reuters/H. Hanschke

Viongozi wa vyama ndugu vya CDU/CSU na chama cha SPD wamekamilisha mkutano wao mjini Berlin wa kuangalia uwezekano wa kuanzisha mazungumzo juu ya kuunda serikali ya msetomiezi mitatu baada ya kufanyika uchaguzi mkuu wa Ujerumani. Awali, Kansela Angela Merkel alisema  vyama hivyo bado vinakabiliwa na vizingiti virefu kwenye mazungumzo hayo vinavyopaswa kuondolewa ili kuweza kufikia makubaliano ya kuunda serikali ya mseto nchini Ujerumani. 

Baada ya mazungumzo ya zaidi ya usiku kucha, muafaka ilifikiwa baina ya pande hizo. Masuala makuu yanayojadiliwa na wajumbe wa vyama hivyo wanaokutana kwenye makao makuu ya chama cha Social Democratic SPD mjini Berlin ni pamoja na uhamiaji, fedha, afya na masuala ya Umoja wa Ulaya.

Kansela Angela Merkel
Kansela wa Ujerumani Angela MerkelPicha: Reuters/H. Hanschke

Kansela Merkel anayefanya juhudi za kuunda serikali mpya ili kuunusuru mustakabali wake wa kisiasa alionya hapo awali kwamba mazungumzo hayo yatakuwa magumu. Baada ya juhudi zake za kuunda serikali na vyama vidogo kushindikana kansela Merkel sasa anaweka matumaini katika washirika wake wa hapo awali wa SPD.

Kiongozi wa chama cha SPD  Martin Schulz
Kiongozi wa chama cha SPD Martin SchulzPicha: Getty Images/AFP/T. Schwarz

Hata hivyo kiongozi wa chama hicho Martin Schulz pia amezungumzia juu ya kuwepo vizingiti vikubwa kwenye mazungumzo hayo, bwana Schulz amesema chama chake kinataka kuhakikisha kwamba serikali mpya itazingatia kwa moyo wote juhudi za kuuimarisha Umoja wa Ulaya. Chama cha hicho cha SPD pia kinataka wafanyakazi wenye vipato vya chini nya vya kati wapunguziwe mzigo wa kodi, hata hivyo hoja hiyo inapingwa na chama cha CSU.

Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier
Rais wa Ujerumani Frank-Walter SteinmeierPicha: picture-alliance/dpa/M. Kappeler

Ili kuyafanikisha mazungumzo hayo rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier amezikumbusha pande zote kwamba zina wajibu wa kuutimiza kwa Umoja wa Ulaya na ameikumbusha kwamba Ujerumani inapaswa kuwa nchi ya kuaminika inayoshiriki katika siasa za kimataifa. Iwapo vyama vya CDU/CSU na SPD havitakubaliana kusonga mbeele na mazungumzo kansela Merkel anaweza kujaribu kuunda serikali ya viti vichache au anaweza kukubali kufanyika uchaguzi mpya.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / Zainab Aziz

Mhariri: Grace Patricia Kabogo