1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mawaziri wa Fedha wa Ulaya wajadili njia za kudhibiti mgogoro wa fedha.

Mohamed Dahman6 Oktoba 2008

Mawaziri wa fedha wa Umoja wa Ulaya waanza mkutano wa siku mbili mjini Luxembourg kupanga mkakati wa kudhibiti machafuko ya kifedha yanayokumba mabenki ya Ulaya kujadli njia za kuongeza usimamizi katika sekta ya fedha.

https://p.dw.com/p/FV1R
Waziri wa Fedha wa Ujerumani Peer Steinbrueck.Picha: AP

Wakati masoko ya hisa yameporomoka kote barani Ulaya maafisa wanakata mapendekzo ya kuunda chombo cha Umoja wa Ulaya kitakachosimamia kila kitu kwa kusema kwamba serikali yumkini zikapendelea kuwepo kwa uratibu wa karibu zaidi wa hatua zitakazochukuliwa na taifa kuzisaidia benki zenye matatizo.

Peer Steinbrück waziri wa Fedha wa Ujerumani akizungumzia mpango wa kuokowa benki ya Ujerumani ya kutowa mikopo ya nyumba Hypo Real Estate anasema:

(O-Ton Steinbrück)

Serikali zaidi za Umoja wa Ulaya zimefuata mfano wa Ujerumani leo hii kutowa hakikisho kwa watu wenye akiba zao mabenki katika juhudi kubwa za kutuliza hofu miongoni mwa wawekezaji juu ya mgogoro huo wa fedha mbaya kabisa kuwahi kushuhudiwa takriban kwa miaka 80.

Hatua hizo zimeshindwa kuyafariji masoko ya fedha.Wawekezaji kuanzia Toyko hadi York wameuza mali zilioko hatarini kwa hofu ya matarajio ya kubanwa zaidi kwa mikopo na utowaji wa mikopo wa mabenki na uwezekano wa kushuka vibaya sana kwa uchumi duniani.

Licha ya juhudi hizo za pamoja kudhibiti mgogoro huo ni wazi kwamba wawekezaji wamekuwa wakitaka kuchukuliwa kwa hatua zaidi na serikali pengine kwa njia ya hatua ilioratibiwa kwa pamoja kutoka katika mkutano wa mwishoni mwa juma lijalo wa Kundi la Mataifa Saba yenye maendeleo makubwa ya viwanda duniani.

Serikali na taasisi za kifedha duniani kote zimekuwa mbioni kurudisha imani kwa vyombo hivyo.

Benki ya Japani imekubali kutowa mkopo wa yeni trilioni 1 sawa na dola bilioni 9.68 kwa mabenki katika mnada wa kuingiza fedha taslimu katika masoko.

Sweden imechukuwa nchi nyengine ya karibuni kabisa katika Umoja wa Ulaya kuchukuwa hatua kwa serikali kusema kwamba itatanuwa akiba za benki na benki kuu kuongeza kima cha mikopo wanachokitowa kwa mabenki.

Hata hivyo hatua ya Ujerumani ya kutowa euro biliono 50 kuokowa Benki ya Ujerumani ya Hypo Real Estate yenye kutowa mikopo ya nyumba na kuchukuliwa kwa Benki ya Uhalinzi na Ubelgiji ya Fortis na Benki Kubwa ya Ufaransa BNP Paribas hakukutiliza sana mashaka yalioko.

Olaf Scholz ni waziri wa kazi wa Ujerumani.

(O-Ton Scholz)

Sote tunawajibika kuhakikisha mfumo wetu wa fedha unafanya kazi kwa jumla na haiwezekani kuachilia hasara itokee na baadae kila mtu anajirusha.

Urusi leo ilisitisha biashara ya hisa kwa saa moja baada baada ya hisa zake kushuka kwa zaidi ya asilimia 14 ambako hakukuwahi kushuhudiwa kwa kipindi cha miaka mitatu wakati hisa za nchi za Ghuba zimeporomoka wakati hofu ikiongezeka kwamba machafuko hayo ya masoko ya fedha barani Ulaya na Marekani yatalikumba eneo hilo.

Benki za Ulaya zimeathiriwa vibaya sana na madhara ya mgogoro huo wa fedha ulioanzia nchini Marekani wakati soko la mikopo ya nyumba lililposambaratika na madeni ya nyumba kuongezeka kupindukia.