1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mashambulizi ya Marekani yauwa watu 19 Syria

Admin.WagnerD25 Septemba 2014

Karibu watu 20 wameuwawa wakiwemo wapiganaji 14 wa itikadi kali na raia watano kufuatia mashambulizi ya anga yanayoongozwa na Marekani dhidi ya kundi linalojiita Dola ya Kiislamu, IS, huko mashariki mwa Syria.

https://p.dw.com/p/1DKuK

Shirika la Uangalizi wa Haki za Binaadamu la Syria limesema usiku wa kuamkia leo, makombora ya anga yalilenga katika maeneo ya visima vya mafuta na kambi ambazo zinadhibitiwa na Dola ya Kiislamu na washirika wa kundi hilo, katika jimbo la mashariki la al-Hasakah na eneo jengine lenye utajiri wa mafuta la Deir al-Zour.

Shirika hilo lenye makao yake makuu mjini London lilieleza kwamba katika eneo hilo kulivurumishwa makombora ya angani kwa takribani mara 12, ambayo yamesababisha vifo vya raia watano, ukiachilia mbali vile vya wanamgambo 14.

Athari za Dola ya Kiislamu

Vile vile ripoti zinasema kwamba mashambulizi mingine ya anga yamefanyika katika eneo la kaskazini la Wakurdi, ambalo limevamiwa na Dola la Kiislamu kwa taribani wiki sasa, na kusababisha zaidi ya watu 150,000 kuyakimbia makazi yao na kuingia mataifa jirani na Syria.

Kurden fliehen vor der IS-Gewalt
Wakurd wanaokimbia mapiganoPicha: DW/Alice Martins

Hata hivyo haijawa wazi nani aliyefanya mashambulizi hayo kwa upande huo wa kusini mashariki mwa Syria kunakojulikana kama Kobani au Ayn Arab.

Wanaharakati katika eneo hilo wanaasema pamoja na kuwepo kwa mashaka ya vifo kuongezeka zaidi, lakini pia wanamgambo wa Dola ya Kiislamu wamewafungulia kiasi ya wafungwa 150 katika gereza moja lililopo katika mji wa Raqqa kaskazini mwa Syria.

kundi la Al-Nusra la Syria shambiliwa

Kundi hilo lenye kujinasibisha kuwa linapiga navita vya kidini limekuwa likiuza mafuta kutoka maeneo hayo katika masoko ya siri kwa ajili ya kuwawezesha kufanikisha operesheni zao. Dola la Kiislamu limedhibiti kwa kasi maeneo makubwa ya uzalishaji wa mafuta nchini Syria tangu mwanzoni mwa mwaka huu.

Aidha duru nyingine zinasema mashambulizi ya anga yalilenga pia kambi za kijeshi za jeshi la Syria zaidi ya 90 ambazo zilitekwa na kundi la Dola ya Kiislamu. Yalilenga mahakama ya Kiislamu na ofisi za kitengo cha utamaduni cha mji wa Mayadeen. Kundi la wapiganaji lenye kutajwa kuwa na mfungamano na mtandao wa al-Qaida, ambalo limekuwa na nguvu kubwa katika mapambano yake dhidi ya kumuondoa Rais Bashar al-Assad, ambalo pia kwa namna fulani limekuwa kipigana bega kwa bega hivi sasa na Dola la Kiislamu limeshambuliwa.

Katika hatua nyengine, Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron ametaka kuhusishwa Iran katika vita dhidi ya Dola la Kiislamu kwa kusema wataweza kuleta umadhubuti Iraq na Syria katika mkutano wake na rais wa Iran, Hassan Rouhani, unaotajwa kuwa wa kwanza kufanyika tangu mapinduzi ya Iran ya mwaka 1979.

Mwandishi: Sudi Mnette AP/DPA
Mhariri: Mohammed Khelef