1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yatuma Silaha Somalia

Jane Nyingi/ AFPE..Picha AFP25 Juni 2009

Silaha hizo zilisafirishwa nchini Somalia kupitia Uganda

https://p.dw.com/p/IbFA
Mwanajeshi wa serikali ya Somalia akishika doria mjini Mogadishu.Picha: AP

Marekani imetuma silaha kwa serikali ya Somalia, baada ya kupata kibali cha ya baraza la usalama la umoja wa mataifa ili kuwazuwia waasi wenye mafungamano na kundi la kigaidi la al-qaeda kutwaa madaraka nchini humo.


Baada Sheikh Sharif Ahmed muislamu mwenye msimamo wa wastani kuwa rais nchini Somalia mwezi Januari, kulikuwa na matumaini hali hiyo ingesaidia kumaliza umwagaji damu ambao umedumu kwa karibu miongo miwili kwa kuridhiana na wenzake wenye msimamo mkali wanaolazimisha kuanzishwa kwa sheria za kiislamu kote nchini humo.


Hata hivyo kiongozi wa mtandao wa kigaidi wa Al-Qaeda Osama bin Laden alimtangaza rais Sheikh Sharif Ahmed adui katika ukanda wa sauti uliotolewa mwezi Marchi mwaka huu wa 2010. Aliwataka wapiganaji kuipindua serikali na waislamu duniani kuunga katika vita vya jihad.


Gazeti la Washington Post limeripoti leo juu ya kutumwa zana za kivita kwa serikali ya Somalia hatua inayoashiria kuwa utawala wa rais Barack Obama unataka kukabiliana na wapiganaji wenye msimamo mkali.


Huku kukiwa na vikwazo cha silaha cha Umoja wa mataifa dhidi ya Somalia ,imearifiwa kuwa baraza la usalama la umoja huo limekubali utaratibu wa silaha mpya kuingizwa nchini Somalia.


Duru nyingine za usalama za nchi za nje zinasema silaha hizo zilisafrishwa nchini Somalia kupitia Uganda, taifa lilichangia nusu ya wanajeshi 4,300 wa Umoja wa Afrika wanaolinda usalama katika maeneo muhimu mjini Mogadishu. idadi iliobakia ni ya wanajeshi kutoka Burundi.

„“Hatari ya kuanguka kwa serikali ya Somalia imesababisha hali ya wasiwasi kwa mataifa ya magharibi, lakini iwapo hatua ya hivi punde itafaulu ni jambo la kusubiri na kuona Rashid Abdi Mchambuzi kutoka shirika la kimataifa la International Crisis Group.„


Kundi la al Shabaab,ambalo linawapiganaji wa kigeni katika usimamizi wake liliimarisha mashambulio yake mapema mwezi Mei mwaka huu.Hivi sasa linadhibiti sehemu nyingi kusini mwa Somali na sehemu kadhaa katika mji mkuu Mogadishu.


Hii leo Alhamis,wapiganaji hao walitumia visu kukata mikono na miguu ya vijana wanne mjini Mogadishu kama adhabu ya wizi, Hiki ni kisa cha kwanza cha ukataji viungo binadamu kutokea nchini Somali.

Kundi la al Shabaab limetekeleza mauaji, kuwachapa watu viboko na ukataji wa kiungo cha mwili hasa katika eneo la Kismayu.Filamu na mpira wa miguu ni mambo yaliopigwa marufuku katika maeneo yanayosimamiwa na wapiganaji wa kundi hilo , na usafiri wa umma wa pamoja wa wanawake na wanaume hauruhusiwi.


Mataifa ya magharibi na baadhi ya mataifa jirani wa Somalia wana wasiwasi huenda waasi wakafanikiwa kuipindua serikali,na taifa hilo kutumiwa kuvurunga hali ya usalama katiaka mataifa jirani zake.




Mwandishi:jane Nyingi /RTRE

Mhariri:Abdul-Rahman