Marekani kuwaondoa wanajeshi wake 5,000 kutoka Ujerumani
2 Mei 2026
Marekani imetangaza kuwa itawaondoa takriban wanajeshi 5,000 kutoka Ujerumani ndani ya miezi 6 hadi 12 ijayo, kulingana na taarifa ya Pentagon iliyotolewa Ijumaa. Hatua hii inakuja wakati Rais Donald Trump akiwa katika mvutano na Kansela wa Ujerumani, Friedrich Merz, kuhusu mkakati wa Marekani katika vita vyake na Israel dhidi ya Iran.
Msemaji wa Pentagon, Sean Parnell, amesema uamuzi huo umetokana na tathmini ya kina ya uwepo wa kijeshi wa Marekani barani Ulaya na mahitaji ya kiusalama katika eneo hilo. Kwa sasa, Marekani ina wanajeshi wapatao 36,000 nchini Ujerumani, hivyo idadi itakayopunguzwa ni karibu asilimia 14.
Waziri wa ulinzi wa Ujerumani, Boris Pistorius amesema leo Jumamosi kwamba, uwepo wa wanajeshi wa Marekani barani Ulaya, na hasa nchini Ujerumani, ni kwa maslahi yao na pia ni kwa maslahi ya Marekani.
Ujerumani ni mwenyeji wa vituo muhimu vya kijeshi vya Marekani, ikiwa ni pamoja na makao makuu ya vikosi vya Ulaya na Afrika, pamoja na kambi ya anga ya Ramstein.
Wachambuzi wanasema uwepo huo unalenga zaidi kulinda maslahi ya Marekani duniani kuliko ulinzi wa moja kwa moja wa Ujerumani.