1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani haitaki zogo na China wala Urusi

Sudi Mnette
29 Aprili 2021

Rais Joe Biden wa Marekani amesema taifa lake litasimama pamoja na China lakini si kwa kutafuta mzozo bali kwa kukaribisha ushindani wenye tija.

https://p.dw.com/p/3siG5
Washington I US-Präsident Joe Biden hält Rede im Capitol
Picha: Jonathan Ernst/REUTERS

Biden ameyasema hayo katika hotuba yake ya kwanza kwa bunge la Marekani, baada ya kutimiza siku 100 tangu aingie madarakani. "Marekani ipo katika hatua ya kusonga mbele tena." Ni sehemu ya maneno ya kutia moyo ambayo ameyasema katika hotuba iliyopindukia takribani saa nzima yenye kugusia masuala ya ndani ya Marekani hadi sera za nje za taifa hilo.

Pamoja na mengine meni Biden, rais wa dola lenye nguvu duniani alisema kwa kufanikisha lengo la ustawi wa biashara zenye usawa duniani, amesema amewahi kumwambia mwenziwe wa China, Xi Jinping kumwambia wazi kuwa wanatafuta ushindani na si mgogoro.

Katika hotuba hiyo ameliomba bunge la taifa kupitisha kiwango kipya cha cha dola trilioni 1.8, ili kuweza kukabiliana na ushindani mkali unaotolewa na China.

Biden ametolea ufafanuzi vikwazo vya Marekani kwa Urusi.

Washington I US-Präsident Joe Biden hält Rede im Capitol
Rais Joe Biden akilihutubia bunge la MarekaniPicha: Jonathan Ernst/REUTERS

Kuhusu vikwazo wa Marekani kwa Urusi, Biden amesema Marekani hatafuti kuchochea mvutano na Rais Vladmiri Putin, isipokuwa ni kutokana na vitendo vya taifa hilo ndivyo vyenye kusababisha wasiwasi. Amesema anaweka wazi kabisa ndivyo vyenye kuleta matokeo hayo. zaidi alisema "Marekani hatuwezi kuupa kisogo wajibu wetu,  wajibu wetu katika haki za binaadamu na ushirikiano wetu. Nilimwambia, hakuna rais wa Marekani anaeweza kukaa kimya kama haki za msingi za binaadamu zinakiukwa waziwazi."

Katika kile kinachoelezwa kuachana kabisa na sera za kigeni za mtangulizi wake Rais Donald Trump, Biden amesema atashirikina kwa karibu na mataifa washirika katika kufuatilia vitisho vinavyosababishwa nan mpango wa nyuklia wa Iran sambamba na Korea Kaskazini.

Vifo vya wazee vinavyotokana na janga la covid 19 vimepungua kwa asilimia 80.

Katika vita dhidi ya janga la Covid-19, Bidenmwenye umri wa miaka 78 alibainisha kwamba tangu Januari, vifo vya wazee vilivyotokana Covid-19 vimepungua kwa asilimia 80. Na kwamba zaidi ya nusu ya watu wenye umri wa utu uzima nchini Marekani wamepata angalau dozi moja ya chanjo.

Katika suala la ubaguzi wa rangi na visa vya mauwaji ya raia wa taifa hilo wenye asili ya Afrika, Biden  amelitaka bunge la taifa hilo kuidhinisha mageuzi makubwa kwa polisi ya Marekani kabla ya Mei 25 ikiwa siku ya kumbukumbu ya kwanza ya kifo cha George Floyd ambae alifariki dunia baada ya kukandamizwa shingini na afisa wa polisi mzungu mwaka jana.

Kiongozi huyo alisema kwa sasa ni wakati wa kuchukua hatua ikiwa ni takribani siku nane baada ya kesi ya Floyd kumalizika na kuhukumiwa kwa mauuji ambae ni afisa wa polisi wa zamani wa Minneapolis Derek Chauvin.

Rais Biden amegusia pia kitisho cha ugaidi akisema vitendo vimevuka mipaka kutoka Afghanistan tangu 2001 na kwamba Marekani itaendelea kuwa madhubuti kuvikabili kokote vilipo. Amesema Al Qaeda na kundi la Dola la Kiislamu wapo Yemen, Syria, Somali na maeneo mengine ya Afrika na Mashariki ya Kati.

Vyanzo: AFP/AP