1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

Mapigano mapya Sudan, UN yatahadharisha hali mbaya ya kiutu

John Juma
1 Mei 2023

Mapigano makali yameendelea Jumatatu kati ya jeshi la Sudan na kikosi cha wanamgambo wa RSF licha ya kurefushwa kwa muda wa makubaliano ya kusitisha vita.

https://p.dw.com/p/4QkL4
Sudan Konflikt l Kämpfe in Darfur l Markt von El Geneina
Picha: -/AFP

Hayo yakijiri, Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuwa hali ya kiutu katika nchi hiyo ipo kwenye ‘ukingo wa kusambaratika'. 

Zaidi ya watu 500 wameuawa tangu mapigano yalipoanza Aprili 15 kati ya jeshi la Sudan linaloongozwa na Abdel Fattah al-Burhan na kikosi chenye nguvu cha Rapid Support Forces (RSF) kinachoongozwa na aliyekuwa naibu mkuu wa majeshi, Mohamed Hamdan Daglo.

Ndege ya kwanza ya Shirika la Msalaba Mwekundu imewasili mjini Khartoum na misaada

Mamilioni ya Wasudan viungani mwa mji mkuu Khartoum wamejificha majumbani mwao, mnamo wakati vyakula, maji na umeme vikizidi kupungua. Ndege za kivita zikiendelea kushambulia, vikosi pinzani pia vimefanya mashambulizi makali ya makombora dhidi ndege hizo. Mkaazi mmoja ameliambia shirika la habari la AFP hayo.

Burhan na Daglo wamekubaliana mara kadhaa kusitisha mapigano kwa muda. Mnamo Jumapili walirefusha makubaliano hayo kwa muda wa saa 72. Hata hivyo makubaliano hayo hayajakuwa yakiheshimiwa huku kila upande ukielekeza lawama kwa mwenzake.

Juhudi za kiutu zaathiriwa

Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuhusiana na hali ya kibinaadamu kufikia hatua ya kutoweza kudhibitiwa.
Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuhusiana na hali ya kibinaadamu kufikia hatua ya kutoweza kudhibitiwa.Picha: Mahamat Ramadane/Reuters

Mamilioni ya Wasudan wamekwama nchini humo, ambako wafanyakazi wa kutoa misaada ni miongoni mwa wale waliouawa.WFP: Machafuko ya Sudan yanaweza kusababisha mgogoro wa kikanda

Vituo vya misaada ya kiutu ni miongoni mwa vituo ambavyo vimeporwa na mashirika ya kigeni yamelazimika kusitisha operesheni zao zote za misaada.

Mkuu wa Haki za Binaadamu wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths alisema Jumapili kwamba anaelekea katika kanda hiyo kusaidia juhudi za dharura za kusambaza misaada kwa mamilioni ya watu ambao maisha yao yamevurugwa ghafla.

Alisema hali ya kiutu imefikia kwenye ukingo wa kusambaratika na kwamba bidhaa za msingi kuwawezesha watu kuendelea kuishi zinazidi kuwa adimu katika maeneo yaliyoathiriwa zaidi, hususan mji mkuu Khartoum.

Griffiths ameongeza kuwa gharama ya usafiri imeongezeka maradufu katika maeneo yanayokumbwa na machafuko, hali ambayo imewaacha wakaazi wengi bila uwezo wa kupata pa kukimbilia.

Maelfu wakimbilia nchi jirani

Waliofanikiwa kukimbia mapigano Sudan wapiga foleni kupokea misaada karibu na mpaka wa Sudan na Chad.
Waliofanikiwa kukimbia mapigano Sudan wapiga foleni kupokea misaada karibu na mpaka wa Sudan na Chad.Picha: Mahamat Ramadane/REUTERS

Takriban watu 50,000 wamekimbia Sudan kufuatia machafuko hayo na kuingia nchi kama Chad, Misri na Jamhuri ya Afrika ya Kati. Hayo ni kulingana na shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa.Mapigano yaendelea Sudan licha ya mkataba wa kuyasitisha

Mapigano hayo yamesababisha raia wa kigeni na waliokuwa wafanyakazi wa kimataifa nchini humo kuondoka kwa wingi, huku nchi mbalimbali zikiwa mbioni kuwaondoa raia wao kwa njia zote ikiwemo ndege, meli na mabasi.

Kikosi cha RSF kinachoongozwa na Daglo kilitokana na kundi la wanamgambo la Janjaweed, lililoanzishwa eneo la Darfur na rais wa zamani aliyepinduliwa madarakani nchini humo Omar al-Bashir.

Mapigano hayo yameenea kote Sudan, ikiwemo Darfur, ambako mashuhuda wameripoti kushuhudia mapigano makali na uporaji.

Chanzo: AFPE