1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni ya wahariri wa magazeti ya Ujerumani.

Abdu Said Mtullya14 Julai 2010

Magazeti ya Ujerumani leo yanazungumzia juu ya mkasa wa mjerumani jasiri Dominik Brunner.

https://p.dw.com/p/OIma
Mnara unaokumbusha kifo cha mjerumani jasiri Dominik Brunner.Picha: dpa


Na leo wahariri wa magazeti wanazungumzia juu ya mkasa wa mjerumani jasiri, juu ya watoto wa wahamiaji nchini Ujerumani na kuhusu mustakabali wa kisiasa nchini Ufaransa.

Vijana wawili leo wanafikishwa mbele ya mahakama katika mji wa Munich kujibu mashtaka ya kumwuua mwananchi mwenzao, Dominik Brunner. Mwananchi huyo jasiri alijaribu kuwatetea watoto wa shule waliokuwa wanabughudhiwa na vijana hao waliomwuua Brunner.

Juu ya kesi hiyo gazeti la Rhein Neckar linasema haidhuru ni hukumu gani itakayotolewa, suala moja linapaswa kuzingatiwa na kuulizwa. Jee jamii ya Ujerumani haioni kuwa imevuna ilichopanda kutokana na kurudi nyuma kila wakati ambapo vijana wanafanya matendo ya kutumia nguvu?

Gazeti la Frankfurter Allgemeine pia linauzungumzia mkasa wa mjerumani huyo jasiri Dominik Brunner aliekufa kutokana na kupigwa wakati akijaribu kuwatetea watoto wa shule.

Gazeti hilo linasema Dominik Brunner ni mtu alieonyesha mfano unaostahili kuigwa.

Lakini mhariri wa gazeti la Frankfurter Allgemeine anasema mahakama inapaswa kuwauliza maswali siyo tu vijana waliompiga na kumwuua Dominik Brunner bali pia inapaswa kuiuliza jamii yote swali moja-jee umoja wa jamii yetu umo katika msingi gani.Jee moyo wa mshikamano una manufaa yoyote?

Gazeti linasema Dominik Brunner ni mtu alieonyesha ujasiri, lakini matokeo ya ujasiri wake yaani kifo yanaweza kuwavunja moyo watu fulani. Kwa hiyo mahakama inayohukumu kesi inayohusu jasiri huyo inapaswa kuipa jamii moyo wa kuwa na mshikamano.

Gazeti la Stuttgarter leo linazungumzia juu ya watoto wa wahamiaji nchini Ujerumani. Gazeti hilo linasema watoto hao wanakabiliwa na matatizo shuleni.Mhariri wa Stuttgarter Zeitung anasema familia ni taifa la Ujerumani linaloelekea katika nasaba za mchanganyiko.

Gazeti hilo linatilia maanani kwamba katika miji mikubwa kama Frankfurt, idadi kubwa ya watoto wana nasaba za uhamiaji. Lakini mhariri anaeleza kuwa katika kila watoto wa shule wanane wa wahamiaji mmoja anamaliza shule bila ya kupata cheti- bila ya kufuzu.

Mhariri wa Stuttgarter anasema idadi hiyo ni ya kutisha sana.Kwa hiyo,mhariri wa gazeti hilo anawataka viongozi walikabili tatizo hilo ,ili kuwaepusha vijana hao na janga la kuwekwa kando ya jamii.

Mhariri wa gazeti la Badisches Tagblatt anatupia macho mustakabali wa kisiasa nchini Ufaransa. Anasema wafaransa wamesimama katika njia panda. Hawajui wapi pa kuelekea.

Mhariri huyo anaeleza kuwa hadi sasa rais Sarkozy amekuwa ni mwanasiasa wa maonyesho badala ya kuwa mtu mwenye maudhui.Na anatambua kwamba hana uwezekano mkubwa wa kuchaguliwa tena katika uchaguzi wa mwaka wa 2012.

Lakini,anasema mhariri wa gazeti la Badisches Tagblatt kwamba wafaransa hawana imani na pande zote za siasa. Gazeti linasema hata kambi ya mrengo wa shoto, ambayo tayari imo katika hali taabani, haina mpango wa kuwapa watu imani.Na hata matatizo ya sasa ya rais Sarkozy hayatakuwa na manufaa kwa kambi hiyo ya mrengo wa shoto ;na kuhusu suala la rushwa na kashfa za michango, kambi hiyo ya mrengo wa shoto inajijua yenyewe iliposimama.

Mwandishi/Mtullya Abdu/Deutshe Zeitungen/

Mhariri/ Abdul-Rahman