1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

...

Abdu Said Mtullya27 Januari 2015

Magazeti ya Ujerumani leo yanatoa maoni juu ya kukombolewa mji wa Kobane nchini Syria, na juu ya serikali ya mseto ya nchini Ugiriki.

https://p.dw.com/p/1EQzQ
Wapiganaji wa Kikurdi wakisherehekea ukombozi wa mji wa Kobane
Wapiganaji wa Kikurdi wakisherehekea ukombozi wa mji wa KobanePicha: picture-alliance/dpa/Str

Gazeti la "Tagesspiegel" linasifu kukombolewa mji wa Kobane wa nchini Syria. Linasema majeshi ya Wakurdi ,Peshmerga yamefanikiwa kuwatimua wapiganaji wa dola la kiislamu na kuukomboa mji huo uliopo kwenye mpaka baina ya Syria na Uturuki.

Mhariri wa gazeti hilo anasema hatimaye harakati za kupambana na dola la kiislamu zinasonga mbele. Lakini mhariri huyo anasema la muhimu zaidi ni kuwakabili magaidi wa dola la kiislamu kaskazini mwa Iraq ,katika mji wa Raqqa ambao magaidi wa dola la kiislamu wanautumia kama makao yao makuu.

Mhariri huyo anasema ni katika mji huo ambapo nguzo ya dola la Kiislamu inapaswa kuvunjwa.Na hapo ndipo mtu anapoweza kusema kwamba ushindi dhidi ya magaidi wa dola kiislamu umepatikana.

Serikali mpya nchini Ugiriki
Gazeti la "Neue Osnabrücker" linatoa maoni juu ya serikali mpya ya mseto iliyoundwa nchini Ugiriki baada ya ushindi wa chama cha mrengo mkali wa kushoto, Syriza. Chama hicho kimeunganisha nguvu na chama cha mrengo mkali wa kulia.

Mhariri wa gazeti la "Neue Osnabrücker"anasema Waziri Mkuu mpya wa Ugiriki Alexis Tsipras ameapishwa kwa kasi ya ajabu ,ili kuanza kazi. Lakini hatua hiyo ya haraka bado haijayatatua matatizo Ugiriki, yaani nchi yenye mzigo mkubwa wa deni. Suala linalovileta pamoja vyama vya Syriza na hicho cha mrengo mkali wa kulia, ni msimamo wa kuipinga sera ya kubana matumizi.La siyvo kila upande una ajenda yake. Ndiyo kusema mvutano mkubwa baina yao ni kama kangaja na upo njiani unakuja.

Ziara ya Obama nchini India


Gazeti la "Märkische Oderzeitung" linaizungumzia ziara ya Rais Barack Obama nchini India kwa kusema kuwa India inapewa umuhimu na Marekani,na hasa kiuchumi .Gazeti hilo linatilia maanani kwamba baada ya muda mrefu wa mvutano, makubaliano yamefikiwa juu ya kushirikiana katika matumizi ya amani ya nyuklia, baina ya India na Marekani.

Gazeti la "Märkische Oderzeitung "linasema umuhimu wa India kijeshi pia unastawi kama mshindani wa China katika bara la Asia, kutokana na mahala ilipo yaani karibu na Afghanistan na Pakistan. Rais Obama anamtilia maanani Waziri Mkuu Modi wa India. Hiyo ni ishara nzuri.

Mwandishi: Mtullya Abdu/ Deutsche Zeitungen

Mhariri: Mohammed Khelef