1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Sanders hataki kubwaga manyanga

Admin.WagnerD9 Juni 2016

Wahariri wanasema Hillary Clinton kimsingi tayari anayo, kibindoni tiketi ya kukiwakilisha chama chake katika uchaguzi wa Rais lakini safari yake bado ni ndefu .Wahariri pia wanatoa maoni juu ya Uingereza

https://p.dw.com/p/1J3bB
Atakaegombea urais ,nchini Marekani Hillary Clinton
Atakaegombea urais ,nchini Marekani Hillary ClintonPicha: Getty Images/AFP/T. A. Clary

Aliesema kwamba safari ya Hillary Clinton bado ni ndefu ni mhariri wa gazeti la " ThüringischLandeszeitung" . Mhariri huyo anaeleza kuwa mshindani wake mkubwa Donald Trump, hatatahayari kusema kila kitu kibaya ,juu ya mama huyo anaekiwakilisha chama cha Demokratik.


Mhariri wa gazeti hilo anasema Trump sio tu mwanasiasa anaeropoka ili kujijengea umaarufu, bali pia amejianika kuwa ni mbaguzi wa rangi na muongo.

Mhariri wa gazeti la "Türingischen Landeszeitung" anatilia maanani kwamba baadhi ya watu wanapenda anayosema Trump,kwa sababu anawananga viongozi wa sasa wa siasa za Marekani, ikiwa pamoja Hillary Clinton.Lakini tatizo ni kwamba Clinton mwenyewe anatoa fursa hiyo. Ajitayarishe kuyasikia mengi katika miezi ijayo. Safari yake bado ni ndefu

Sanders hataki kubwaga manyanga

Mhariri wa gazeti la "Emder" anasema kimsingi ,kinyang'anyiro cha kuwapata wagombea urais kimemalizika. Ni Clinton kwa upande wa Democratik na Trump kwa upande wa Republican. Lakini mhariri huyo anasema pana tatizo. Bernie Sanders, mshindani wake Clinton na anaeleza.


Ingawa Hillary Clinton ameshafikia idadi ya wajumbe anaowahitaji ili kukiwakilisha chama chake cha Demokratik katika uchaguzi wa rais, mshindani wake kutoka chama hicho hicho Bernie Sanders hataki kubwaga manyanga! Bado anataka kuyanadi mawazo yake mbele ya mkutano mkuu wa chama hicho utakaofanyika Philadelphia.

Bernie Sanders asema mapambano yanaendelea
Bernie Sanders asema mapambano yanaendeleaPicha: Getty Images/S. Olson


Mhariri wa gazeti la "Emder" anasema tunapaswa kumpongeza Bernie Sanders kwa kampeni aliyoendesha na hasa kuhusu suala la kuwatetea masikini.Lakini lingekuwa shauri bora kwa Sanders kuisimamisha kampeni yake. Chama cha Demokratik,sasa lazima kijinoe kwa ajili ya kupambana na Donald Trump.

Mhariri wa gazeti la " Bild " anasema mpaka sasa watu wanazijadili hoja zinazotolewa na kila upande nchini Uingereza , juu ya nchi hiyo kuendelea kuwemo katika Umoja wa Ulaya au kujitoa. Lakini mhariri huyo anasema watu wanasahau kwamba ,yatakuwa maafa makubwa kwa Umoja wa Ulaya, ikiwa Uingereza itajiondoa kwenye jumuiya hiyo.

Wazawa pia ni wahalifu
Ofisi kuu ya kupambana na uhalifu nchini Ujerumani BKA imechapisha ripoti juu ya uhalifu uliotendwa na wahamiaji katika majimbo yote 16 ya Ujerumani. Kwa mujibu wa ripoti hiyo,wahamiaji walifanya vitendo vya kihalifu,alfu 69 katika miezi mitatu ya kwanza ya mwaka huu.

Juu ya ripoti hiyo mhariri wa gazeti la "Rhein-Zeitung anakiri kwamba wakimbizi wanatenda uhalifu, lakini anasema kwa wastani siyo kupita wazawa wa nchi.

Mwandishi:Mtullya abdu/Deutsche Zeitungen.

Mhariri: Yusuf Saumu