1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maoni: Hofu ya mfumo wa vyama vingi Afrika 2017

Claus Stäcker28 Desemba 2016

Mwaka 2016 haukuwa wa ufanisi kwa bara la Afrika. Hali ya kiuchumi imedhoofika, vijana wanapiga kura kuchagua mageuzi, lakini hawayapati, anasema mkuu wa idhaa zinazozitangazia nchi za Afrika kutoka DW, Claus Stäcker.

https://p.dw.com/p/2UyF2
Karte Afrika Übersicht
Picha: DW

Mwalimu wa zamani wa hesabu, Faustin Touadéra, angeweza kuwaletea matumaini Waafrika. Uchaguzi uliokuwa ukisubiriwa kwa muda mrefu katika Jamahuri ya Afrika ya Kati, ulimalizika kwa kumpatia ushindi Febuari 14 na kwa namna hiyo kuzusha matumaini ya kuibuka mwaka mwema barani Afrika.

Hata hivyo furaha haijakawia kutoweka. Hakuna mengi ya kutia moyo, yaliyochomoza barani Afrika mwaka 2016. Siku nne tu baada ya kuchaguliwa Touadéra, utepe laini wa matumaini ukakatika pale rais wa muda mrefu wa Uganda Yoweri Museveni, alipojihakikishia muhula wake wa tano madarakani kwa kuwatumilia nguvu na kuwatenga wapinzani wake.

Katika hali kama hiyo pia amechaguliwa, Idriss Déby, aendelee na muhula wa tano madarakani kama rais wa Chad. Na mwezi Agosti rais wa Gabon, Ali Bongo, akatanagazwa mshindi kwa kujikingia kura 6,000 tu zaidi.

Jirani na huko, rais wa nchi tajiri kwa gesi na mafuta wa Guinea ya Ikweta, Teodoro Obiang Nguema, aliyejipatia asili mia 93.7 anaendelea na muhula wa sita madarakani, hakuna yeyote aliyetanabahi ulimwenguni. Hata mpinzani wa demokrasia, Pierre Nkurunziza, nchini Burundi ametoweka katika rada za jumuia ya kimataifa na kuimarisha kichini chini madaraka yake.

Na Ethiopia nayo bado inasubiri. Kizazi kipya kilichojaa matumaini kina kiu cha kuchangia katika mfumo wa nguvu wa kidemokrasia na wa kiuchumi. Kishindo kikubwa kinawakaba viongozi wa chama tawala "Chama cha Mapinduzi ya Kidemokrasi ya Umma wa Ethiopia - EPRDF," ambao baada ya machafuko na matumizi ya nguvu ya mwezi wa Oktoba, hawajapata njia nyengine isipokuwa kutumia sheria ya hali ya hatari. Kwamba maelfu wataachiwa huru mwaka huu utakapomalizika, hilo pengine linatokana zaidi na mtazamo wa busara.

Stäcker Claus Kommentarbild App
Mkuu wa idhaa zinazozitangazia nchi za Afrika kutoka DW, Claus Stäcker

Viongozi wawili waliobebeshwa matumaini mwaka 2016, nuru yao imefifia, ambao ni: Rais Muhammadu Buhari wa Nigeria, na John Magufuli wa Tanzania. Na wote wawili, hawakukidhi matumaini waliyowekewa.

Buhari anakorogwa na sheria na kujitokeza mara nyingi kana kwamba hajaarifiwa ipasavyo. Na Magufuli anaonekana kuendesha vita vya upande mmoja na kuwafanya wadau wa vyombo vya habari, mashirika ya kirais, sheria na mpaka wale wanaopigania demokrasia kumgeukia.

Hali si afadhali nchini Afrika Kusini. Kashfa zinazoigubika serikali kuhusu mawaziri wanaohongwa, na makubaliano ya kinamna namna ya ngazi ya juu yanatishia kuigeuza nchi hiyo kuwa nchi isiyofuata sheria. Vuguvugu kongwe kabisa la ukombozi barani Afrika - Chama cha African National Congress - ANC kilichoundwa miaka 105 iliyopita, kinaonyesha kushindwa kujifanyia marekebisho.

Mageuzi barani Afrika yanawezekana kupitia kwa Waafrika wenyewe. Sawa na ilivyowezekana nchini Ghana ambako, Nana Akufo-Addo, amechaguliwa kuwa rais wa nchi hiyo. Viongozi wa kisiasa wanabidi waachane na hofu dhidi ya mfumo wa vyama vingi. Mashindano ya kisiasa na kiuchumi yanabidi yaangaliwe kuwa ni kitu cha kawaida. Sio katika kila uchaguzi linazuka suala la kufa kupona - ni suala la mashindano ya amani ya fikra na imani kwa nchi na taasisi zake.

Katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Joseph Kabisa, fikra hiyo haijamwingia akilini. Muimla wa Gambia, Yahya Jammeh, anaweka mtego akidhamiria kubadilisha mfumo wa kupiga kura.

Alichokisema kimemgeukia. Hakuna ajuae nini kitatokea Januari 19, siku iliyopangwa kukabidhi madaraka. Matumaini ya vijana yako pia Kenya ambako uchaguzi muhimu kabisa utaitishwa mwaka 2017. IShara ni moja tu, nayo ni kwamba sauti ina thamani, kuanzia katika kituo cha kupiga kura mpaka nje ya kituo hicho.

Mwandishi: Claus Stäcker/Hamidou Oummilkheir

Mhariri: Grace Patricia Kabogo